

9 April 2025, 15:14 pm
Huu ni msisitizo kwa wakulima kuhakikisha wanalima kilimo mchanganyiko kwenye zao la Korosho ili kusaidia kupunguza ghalama za upaliliaji pamoja na kuongeza virutubisho vinavyotokana na mazao yanayochanganywa kwenye mikorosho hiyo.
Na Musa Mtepa
Wakulima wa zao la korosho nchini wamehamasishwa kulima kilimo mchanganyiko wa mazao ya msimu ili kusaidia kurudisha gharama za upaliliaji na kuongeza virutubisho vinavyohitajika katika udongo wa shamba la korosho.
Mazao ya msimu ambayo yanafaa katika kilimo mchanganyiko (intercropping) na korosho ni pamoja na Karanga, Kunde, Ufuta, Njugu mawe, Choroko, na jamii nyingine za kunde.
Wito huo umetolewa na Mtafiti kiongozi wa Programu ya Zao la Korosho na Mratibu wa Utafiti na Ubunifu kutoka Kituo cha Utafiti wa Kilimo TARI Naliendele, Dr. Wilson Nene, tarehe 8 Aprili, 2025.
Dr. Nene amesema kuwa uchanganyaji wa mazao ya msimu kwenye shamba la korosho kuna manufaa makubwa, ikiwemo kurudisha faida za gharama za kuanzisha shamba la korosho kwa muda mfupi.
Aidha amesema kuwa mazao ya msimu yanaweza kusaidia kuimarisha ardhi, kupunguza gharama za uzalishaji, na kuongeza kipato cha wakulima.
Aidha, Dr. Nene ameongeza kuwa kilimo mchanganyiko kinaweza pia kupunguza uhamaji wa wakulima kutafuta rutuba ya ardhi, kwani husaidia kurejesha rutuba iliyopotea kutokana na kilimo cha monokultura.
Baadhi ya wakulima kutoka kata ya Naliendele wameelezea faida za kilimo mchanganyiko, na wamewataka wakulima wengine kuiga njia hii kutokana na manufaa inayopatikana.
Wakulima hao wamesema kuwa, pamoja na kuimarisha tija ya kilimo cha korosho, kilimo mchanganyiko kinawafaidi kwa kuongeza mapato yao na kupunguza utegemezi wa mazao moja.
Kwa hivyo, ni muhimu kwa wakulima wa korosho nchini kuzingatia kilimo mchanganyiko, kwani ni suluhisho la kusaidia kuboresha uzalishaji na kuongeza tija katika sekta ya kilimo.