FM Manyara

Aliyekuwa mwalimu mkuu Ufana, kortini kwa tuhuma za kughushi nyaraka

11 September 2026, 5:57 pm

Picha ya mahakama ya wilaya ya Babati

Aliyekuwa Mwalimu Mkuu wa Shule ya Sekondari Ufana wilayani Babati mkoani Manyara Paulo Stephen Mapunda, amefikishwa katika Mahakama ya Wilaya ya Babati, akikabiliwa na jumla ya makosa 12, yanayohusiana na kughushi  nyaraka za malipo na matumizi ya fedha za shule.

Na Mzidalfa Zaid

Kesi hiyo imesikilizwa mbele ya Hakimu Mkazi Mwandamizi wa Mahakama ya Wilaya ya Babati, huku upande wa Serikali ukiwakilishwa na Mawakili wa Serikali kutoka TAKUKURU, Neema Gembe na Davis Masumbu ambao wamesema Mshitakiwa alitenda makosa hayo kati ya December 12 2024 Hadi February 28 2025.

Kwa mujibu wa maelezo yaliyotolewa mahakamani hapo  Mapunda anatuhumiwa kufanya makosa ikiwemo kughushi nyaraka na hati za malipo, pamoja na kutumia nyaraka hizo katika mchakato wa  matumizi ya fedha kiasi cha shilingi milioni tano na elfu themanini na tano (5,085,000) kupitia akaunti ya shule kwa matumizi binafsi.

Kesi hiyo imeahirishwa Hadi September 17 na Mshitakiwa amekana kesi inayomkabili na amepata dhamana baada ya kukidhi vigezo vya kuwa na wadhamini 2 ambao wamesaini hati ya dhamana million 10.