FM Manyara
FM Manyara
5 June 2026, 6:34 pm

Shirika la Civic Social Protection Foundation (CSP) kwa kushirikiana na Vi Agroforestry limeadhimisha Siku ya Mazingira Duniani kwa kutekeleza shughuli mbalimbali za uhifadhi wa mazingira katika Halmashauri ya Mji Babati, mkoani Manyara.
Na Mzidalfa Zaid
Akizungumza wakati wa maadhimisho hayo, Mwanasheria wa CSP, Eliakim Paul, amesema taasisi hiyo imeendelea kushirikiana na jamii katika juhudi za kulinda mazingira kupitia upandaji miti, elimu ya mazingira na shughuli za usafi.
Amesema katika maadhimisho ya mwaka huu jumla ya miti 1,200 ya matunda, mbao na kivuli imepandwa katika maeneo mbalimbali yakiwemo Shule ya Msingi Malangi, Zahanati ya Malangi, Shule za Sekondari FT Sumaye na Himiti pamoja na ofisi ya kijiji cha Himiti.
Mgeni rasmi katika shughuli hiyo alikuwa ni Aretas Laurent aliyemwakilisha Afisa Mazingira wa Mkoa wa Manyara ambapo amewahamasisha wananchi kuendelea kupanda miti na kufanya usafi wa mazingira mara kwa mara ili kukabiliana na changamoto za mabadiliko ya tabianchi na kulinda mazingira kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.

