FM Manyara
FM Manyara
24 July 2026, 7:19 pm

Mfumo wa kidijitali wa kuwaunganisha wakulima, wafanyabiashara na wadau wa mazao ya mikunde umezinduliwa mkoani Manyara, ukiwa na lengo la kuwasaidia wakulima kupata taarifa sahihi za masoko, bei za mazao pamoja na fursa mbalimbali katika mnyororo wa thamani wa mikunde.
Na Mzidalfa Zaid
Mratibu wa Mtandao wa Mfumo wa Kidijitali wa Wadau wa Mazao ya Jamii ya Mikunde Tanzania Zirack Andrew, amesema mfumo huo utawasaidia wakulima na wafanyabiashara kufahamu bei za mazao kwa wakati, kupata taarifa mbalimbali za kilimo pamoja na kuunganishwa na masoko yenye uhakika.
Amesema mfumo huo pia utarahisisha kuunganisha wadau wote wa mnyororo wa thamani, kuongeza ushirikiano baina yao, kukuza biashara ya mazao ya mikunde pamoja na kuongeza kipato cha wakulima.

Kwa upande wake, Makamu Mwenyekiti wa Chama cha Wakulima wa Alizeti Tanzania ambaye pia ni mfanyabiashara wa mazao Athuman Karunde, amesema mfumo huo utarahisisha upatikanaji wa mazao yenye ubora, kuongeza uaminifu kati ya wakulima na wanunuzi, pamoja na kuboresha biashara ya mazao ya kilimo.

Afisa Ushirika Mkoa wa Manyara Godamen Merinyo ambae alikuwa mgeni rasmi katika uzinduzi huo ,amesema teknolojia hiyo ni fursa muhimu kwa wakulima kupata masoko ya uhakika, kuongeza kipato na kuimarisha maendeleo ya sekta ya kilimo kupitia matumizi ya mifumo ya kidigitali.

Nao baadhi ya wakulima kutoka maeneo mbalimbali ya Mkoa wa Manyara wamesema kabla ya kuanzishwa kwa mfumo huo walikuwa wakikabiliwa na changamoto ya kukosa taarifa sahihi za masoko na kuwauzia walanguzi mazao yao kwa bei ya chini.