FM Manyara

Wananchi Babati watakiwa kuchangamkia matibabu bure

17 September 2026, 9:15 pm

Picha ya mkurugenzi wa halmashauri ya wilaya ya Babati Anna mbogo (kulia) picha na Marino Kawishe

Wananchi wilayani Babati mkoani Manyara wametakiwa kuchangamkia fursa ya matibabu bure

Na Marino Kawishe

Zikiwa zimesalia siku mbili kabla ya kumalizika kwa kambi ya afya inayotoa huduma za matibabu katika baadhi ya kata wilayani Babati, mkoani Manyara, wananchi wametakiwa kuchangamkia fursa hiyo ya matibabu bure kabla ya kambi hiyo kufungwa Jumamosi, Septemba 19, mwaka huu.

Akitoa tathmini ya ziara yake katika kambi hiyo, Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Babati, Anna Mbogo, amelishukuru shirika la So They Can Tanzania pamoja na wadau wote walioshirikiana na madaktari kutoka Hospitali ya Wilaya ya Babati katika kutoa huduma mbalimbali za afya kwa wananchi.

Sauti yaMkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Babati, Anna Mbogo
Picha ya mkurugenzi wa halmashauri ya wilaya ya Babati akifanyiwa uchunguzi wa kiafya

Aidha, Mbogo amewataka wananchi wa kata zilizobaki ambazo ni Endakiso na Mamire kujitokeza kwa wingi kupata huduma hizo za afya ambazo zinatolewa bure, huku akiwataka kuachana na dhana ya kusubiri siku ya mwisho ya kambi, hali ambayo inaweza kuwafanya baadhi yao kukosa huduma.

Katika ziara hiyo, Mkurugenzi huyo ametembelea kambi ya afya iliyopo Kata ya Qash, ambapo pia alipata fursa ya kupata huduma za uchunguzi wa macho na masikio.