FM Manyara
FM Manyara
17 August 2026, 12:47 pm

Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Queen Sendiga, leo amezindua tisheti rasmi zitakazotumika katika mbio za hisani za Manyara Tanzanite Marathon, zinazotarajiwa kufanyika Agosti 22 mwaka huu.
Na Mzidalfa Zaid
Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Sendiga amesema hadi kufikia asubuhi ya leo, jumla ya watu 2,200 wamekwishajisajili kushiriki katika mbio hizo za hisani, huku wananchi 123 wakijisajili kushiriki katika utalii wa ndani kwa kutembelea Hifadhi ya Taifa ya Tarangire.
Kwa upande wake, Mganga Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Dkt. Andrew Method, amesema mwitikio wa wananchi katika kushiriki mbio hizo umekuwa mkubwa, huku akiwataka wananchi ambao bado hawajajisajili kutumia fursa hiyo kujiandikisha, na wale ambao tayari wamejisajili kuendelea kuchukua tisheti zao za mbio hizo.
Nao baadhi ya washiriki waliopokea tisheti hizo wamesema wameshiriki katika mbio hizo kwa lengo la kuimarisha afya zao, pamoja na kuchangia katika kuokoa maisha ya watoto wachanga, hususan watoto njiti.
Manyara Tanzanite Marathon inatarajiwa kufanyika Agosti 22 mwaka huu, huku mgeni rasmi akitarajiwa kuwa Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mwigulu Nchemba. Mbio hizo zinafanyika chini ya kaulimbiu isemayo “Hatua Moja, Okoa Maisha ya Mtoto.”
