Jamii FM
Jamii FM
18 July 2025, 11:08 am

Wasimamizi wa uchaguzi Lindi na Mtwara wamehimizwa kuzingatia Katiba, sheria na kanuni kuelekea Uchaguzi Mkuu 2025. Mafunzo ya siku tatu yamehitimishwa Mtwara, yakilenga kuwajengea uwezo. Washiriki wameahidi kuwa mabalozi wa elimu hiyo kwa wenzao
Na Musa Mtepa
Wasimamizi na waratibu wa uchaguzi kutoka mikoa ya Lindi na Mtwara wametakiwa kuhakikisha wanazingatia katiba, sheria na kanuni za uchaguzi katika hatua zote za maandalizi na utekelezaji wa Uchaguzi Mkuu unaotarajiwa kufanyika Oktoba 2025.
Wito huo umetolewa July 17, 2025 na Bi Sesilia Sepanjo, Mratibu wa Mafunzo ya uchaguzi, wakati wa kufunga mafunzo ya siku tatu yaliyofanyika katika ukumbi wa Benki Kuu, tawi la Mtwara. Mafunzo hayo yalilenga kuwajengea uwezo wasimamizi hao kuelekea uchaguzi mkuu ujao.
Aidha, Bi Sepanjo amewahimiza wasimamizi kutumia vyombo vya habari kama jukwaa la kuwaelimisha wananchi na wadau wengine kuhusu masuala muhimu yanayohusu uchaguzi, ili kuongeza uwazi na uelewa kwa jamii.
Pia Bi Sepanjo amewasisitiza wasimamizi na waratibu wa uchaguzi kupunguza matumizi ya vikundi sogozi vya WhatssAp ili wasije kosea kutuma taarifa yeyote katika makundi hayo ambayo hayakutakiwa kutuma huko.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Mafunzo hayo, Daudi Muharagi, amesema washiriki wamefundishwa zaidi ya mada 12 muhimu zinazohusu uchaguzi, akisisitiza kuwa maarifa hayo yanapaswa kutumika kwa weledi na kwa manufaa ya taifa.

Washiriki wa mafunzo hayo, akiwemo Bi Kidawa Mohamed na Bw. Winfridi Tamba, wameeleza kuwa mafunzo yamewasaidia kuongeza uelewa kuhusu taratibu na hatua mbalimbali za uchaguzi na kualiahidi kuwa mabalozi wazuri wa kusambaza elimu hiyo kwa wenzao ili kuhakikisha ufanisi na usawa katika zoezi hilo muhimu la kitaifa.
