Nuru FM

Muundo Wa Mitaala Waanza Kuandaliwa

23 March 2022, 7:42 am

Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia (WyEST) na Wizara ye Elimu na Mafunzo ya Amali (WEMA) kupitia Taasisi ya Elimu Tanzania (TET) na Taasisi ya Elimu Zanzibar (TEZ) imekamilisha zoezi la kuchambua maoni ya wadau pamoja na kuandika ripoti ya hali ya sasa kuhusu mahitaji ya uboreshaji wa mitaala yaani situational analysis report.

Mkurugenzi Mkuu wa TET Dkt.Aneth Komba amesema kwa sasa kamati ya wataalamu (technical committee) inayosimamia kazi ya maboresho ya mitaala iliyoteuliwa na Waziri wa Elimu Prof. Adolf Mkenda imekutana Mjini Morogoro kwa kikao kazi cha siku 6 kuanzia tarehe 21 hadi 26, Machi 2022.

Amesema kuwa lengo la kikao kazi hicho ni kuchambua ripoti ya maoni ya wadau, maandiko mbalimbali na uzoefu kutoka nchi nyingine ili kutengeneza muundo wa mitaala ya elimu ya Awali, ElimuMsingi, Sekondari na Ualimu. Muundo huu ndio utakaotumika kuandaa Mitaala tajwa.

Ameeleza pia kikao kazi hicho kinaongozwa na Mwenyekiti wake Prof.Makenya Maboko pamoja na wajumbe kutoka vyuo vikuu, Wizara, TET, TEZ na wataalamu kutoka sekta binafsi.