Mpanda FM

Wazazi, walezi Katavi watakiwa kuwafundisha maadili mema watoto

29 September 2024, 8:36 am

Mkuu wa Mkoa wa Katavi Mwanamvua Mrindoko na baadhi ya wananfunzi ambao wamefika katika uzinduzi wa tuwaambie kabla hawajaharibiwa .picha na John Mwasomola

“Walimu pamoja na wazazi wanatakiwa kuweka ulinzi mkubwa kwa Watoto ili kujenga taifa moja litakalokuwa na kizazi chenye maadili mema.”

Na John Mwasomola -Katavi

Wazazi na walezi mkoani Katavi wametakiwa kuwalinda watoto na kuwafundisha maadili yanayofaa ili kuwaepusha na vishawishi mbalimbali.

Wito huo umetolewa na Kamanda wa Jeshi la Polisi Mkoa wa Katavi Kaster Ngonyani wakati wa uzinduzi wa kampeni ya tuwaambie kabla hawajaharibiwa iliyofanyika katika viwanja vya Polisi Buzogwe mkoani Katavi.

Ngonyani amesema kuwa jeshi la polisi kwa kushirikiana na dawati la jinsia, walimu pamoja na wazazi wanatakiwa kuweka ulinzi mkubwa kwa watoto ili kujenga taifa moja litakalokuwa na kizazi chenye maadili mema.

Sauti ya Kamanda wa jeshi la Polisi Mkoa wa Katavi Kaster Ngonyani

Kwa upande wake Mkaguzi wa Polisi Judith Mbukwa ambaye ni Mkuu wa Dawati la Jinsia na Watoto Mkoa wa Katavi amewaasa wananchi kutoogopa kwenda kutoa taarifa za matukio yanayohusiana na ukatili wa kijinsia kwa kuwa hiyo ndiyo kazi ya jeshi la polisi kushirikiana na wananchi kutokomeza vitendo hivyo.

Sauti ya Mkaguzi wa Polisi Judith Mbukwa ambaye ni Mkuu wa Dawati la Jinsia na Watoto Mkoa wa Katavi

Mmoja wa wanafunzi ambao wameshiriki katika kampeni hiyo amewasihi wazazi kutowafanyia watoto vitendo vya kikatili ili kufanikiwa katika mambo yao, pia amewataka watoto kuendelea kujiamini na kutokubali kushawishika.

Sauti ya mwanafunzi akizungumza

Mkuu wa Mkoa wa Katavi Mwanamvua Mrindoko ambaye alikuwa mgeni rasmi ametumia fursa hiyo kuwataka wazazi na walezi kuwa makini na watoto wao juu ya matumizi ya simu kwani baadhi yao wanajifunza matendo yasiyofaa kupitia simu zao.

Sauti ya mkuu wa mkoa wa Katavi Mwanamvua Mrindoko

Kampeni ya tuwaambie kabla hawajaharibiwa ni kampeni ya nchi nzima ambapo katika mkoa wa Katavi kampeni hiyo imefanyika katika viwanja vya Polisi Buzogwe na mgeni rasmi alikuwa Mkuu wa Mkoa Mwanamvua Mrindoko.