Nuru FM

Mwenyekiti Apora Ardhi Za Wananchi wa Mgera Mkoani Iringa,Atishia Kuwaua Wakilalamika

5 October 2022, 5:16 am

Wananchi wa Kijiji cha Mgera kata ya Kiwele wilaya ya Iringa wamemlalamikia mwenyekiti wa Kijiji hicho kwa kuwapora ardhi ya wananchi kwa kutumia mabavu na madaraka aliyonayo ya kiungozi.

Akizungumza kwenye mkutano wa mkuu wa wilaya ya Iringa Mohamed Hassan Moyo wa kupokea malalamiko ya wananchi, wananchi hao walisema kuwa mwenyekiti huyo amekuwa akiwanyanyasa na kuongeza serikali ya Kijiji kwa mabavu.

Ayubu Mtweve ni mwananchi wa Kijiji hicho alisema kuwa mwenyekiti wa Kijiji Lucas Mgata amempora ardhi yenye zaidi ya hekari mbili ambazo anamiliki kwa zaidi ya miaka thelathini(30) jambo ambalo linawashangaza wengi.

Mkuu wa Wilaya ya Iringa Mohamed Moyo akizungumza na wananchi wa Mgera

Mtweve alisema kuwa mwenyekiti huyo amekuwa anajihusisha kwenye migogoro ya ardhi kwa kupora ardhi za wananchi kwa asilimia kubwa kutokana na kutumia madaraka vibaya aliyonayo.

Alisema kuwa amelalamika kila kona lakini hakuna kiongozi yeyote aliyefanikiwa kutatua mgogoro huo jambo ambalo lilimfanya yeye na wenzake kuandamana hadi ofisi ya mkuu wa wilaya ya Iringa Mohamed Hassan Moyo ili awasaidie kutatua mgogoro huo wa ardhi baina ya wananchi na mwenyekiti huyo.

Mtweve alisema kuwa mwenyekiti huyo anatumia mabavu kupora ardhi za wananchi Jambo ambalo linawafanya wananchi wa Kijiji cha Mgera kukosa amani ya kuishi na kumiliki ardhi.

Mwenyekiti wa Kijiji cha Mgera Lucas Mgata anayelalamikiwa na wananchi wa kijiji Chake kupora ardhi

“Yaani anapora ardhi halafu ukianza kufuatilia anatishia kukuuwa na kukuweka ndani jambo wananchi wengi wamekuwa waoga kufuatilia haki zao hivyo nilipoanza kufutilia bila uoga ndipo wananchi wengine wanajitokeza kulalamika hadi kufika kwa mkuu wa wilaya”alisema Mtweve.

Veronica Chusi ni bibi mwenye umri wa miaka 84 anamlalamikia mwenyekiti wa Kijiji hicho Lucas Mgata kwa kupora ardhi yake kwa njia ya kuazima ardhi aitumie kwa kilimo lakini baadae akaifanya ikawa ya kwake jambo ambalo anasema kuwa kupora ardhi kwa kutumia mabavu.

 

Chusi alisema kuwa ameanza kuitumia ardhi hiyo kabla ya mwenyekiti huyo hajazaliwa iweje leo anasema ya kwake na ameridhishwa na wazazi wake Jambo ambalo sio la kweli hivyo toka ameingia madarakani kiongozi huyo amekuwa na tabia ya kupora ardhi kwa Wananchi.

Bibi huyo alienda mbalimbali zaidi na kusema ukilalamika anakutishia kukuua jambo ambalo linawafanya wananchi wengi kuacha kufuatilia haki zao.

“Mwenyekiti anwike ardhi yetu kwakutumila nguvu,pe mwana mdodo atufile bahaa akutuanuka ilieneo letu iserikali twisuka mtange tuvayenu tufayenu tunamiaka zaidi ya themanini tugapakuliwa tutegemee bahaa”, alisikika Mzee huyo akiongea kwa lugha ya kihehe na kiswahili kuomba msaada wa kusaidia kutatua mgogoro huo.

Bibi Chusi alimazia kwa kusema kuwa ukifika Kijiji hapo ukimuuliza kila wananchi atakuambia kuhusu uporaji wa ardhi anaoufanya mwenyekiti huyo wa Kijiji kwa kuwa sio kificho Tena.

Bibi Veronica Chusi mwenye umri wa miaka 84 anayelalamika kuporwa ardhi yenye ukubwa Hekari 2 na Mwenyekiti wa Kijiji chao

Naye bibi Lusia Mbugano mwenye umri wa miaka 90 alisema kuwa mwenyekiti huyo amekuwa akiwanyanya ardhi Mara kwa mara na walikuwa wanakaa kimya kutokana na kutishiwa amani na kiongozi huyo.

Bibi Mbugano alisema kuwa mara ya kwanza aliwapora ardhi ambayo waliachiwa urithi na marehemu baba yai Mzee Mwesimpya Nyaulingo miaka ya 1937 huko lakini kiongozi huyo amekuwa akitumia njia mbalimbali ikiwemo kuwatishia kupora ardhi.

Alisema kuwa hivi sasa hana hata eneo la kulima kutokana na kupora maeneo yote na mwenyekiti huyo wa Kijiji cha Mgera hivyo ameiomba serikali kusaidia kutatua mgogoro huo.

Bibi Mbugano alisema kuwa hivi karibu mwenyekiti huyo amempora tena ardhi ya hekari tatu ambazo alikuwa amebakiwa nazo hivyo unakaribia wakati wa kilimo na hana eneo la kulima anaiomba serikali kuharakisha kutatua mgogoro huo.

Kwa upande wake mwenyekiti wa Kijiji cha Mgera Lucas Mgata alisema kuwa tuhuma zote alizopewa na wananchi sio za kweli na wanamsingizia tu kutokana na utendaji wake wa kazi.

Mohamed Hassan Moyo ni mkuu wa wilaya ya Iringa alilazimika kufika katika eneo lenye mgogoro huo wa ardhi na kubaini kuwa kunamgogoro ambao unatakiwa kutatuliwa haraka.

Moyo alisema kuwa atatuma wataalam kuchunguza malalamiko ya wananchi wa kijiji cha Mgera wanaodai kuwa Mwenyekiti wa Serikali ya kijiji chao amekuwa chanzo cha migogoro kwa kupora maeneo ya ardhi ya Wananchi

Alitoa kauli hiyo baada ya wananchi kudai kuwa mwenyekiti wao amezusha hofu katika kijiji hicho baada ya kujimilikisha ardhi isivyo halali maeneo yenye makazi ya watu pamoja na mashamba.

Moyo aliyefika katika maeneo yenye mgogoro amebaini kuwa walalamikaji pamoja na mlalamikiwa , wote hawana hati za umiliki wa ardhi hiyo hivyo amepiga marufuku kufanyika kwa shughuli zozote hadi ufumbuzi utakapopatikana

 

CREDIT FRED MGUNDA