Joy FM
Joy FM
14 June 2025, 10:08

Serikali imesisitiza wananchi kutumia vyandarua kwa matumizi yaliyokusudiwa ili waweze kujikinga na ugonjwa wa Malaria
Na Hagai Ruyagila
Mkuu wa Wilaya ya Kasulu, Kanali Isaac Mwakisu, amevitaka vyombo vya ulinzi na usalama wilayani humo kuhakikisha vinafuatilia na kubaini wananchi wanaouza vyandarua nje ya nchi ili waweze kuchukuliwa hatua za kisheria
Kanali Mwakisu ametoa agizo hilo wakati wa hafla ya uzinduzi wa kampeni ya ugawaji wa vyandarua ngazi ya kaya bila malipo, iliyofanyika katika uwanja wa Utamaduni Mjini Kasulu Mkoani Kigoma.
Amesema zaidi ya vyandarua Laki nne vimeaza kugawiwa katika wilaya ya hiyo huku akiwasisitiza wananchi kuvitumia kwa kujilinda dhidi ya mbu wanao sababisha ugonjwa wa malaria pamoja na kuvitaka vyombo vya ulinzi na usalama kuchukua hatua kwa mwananchi yeyote atakaye kitumia chandarua hicho kinyume na utaratibu uliopangwa.
Mganga Mkuu wa halmashauri ya Mji Kasulu Dkt Peter Janga amesema kiwango cha vifo vitokanavyo na ugonjwa wa malaria imeendelea kupungua kwa kiwango cha juu.
Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji Kasulu Mwl. Vumilia Simbeye ameishukuru seriakali kwa namna inavyowajali wananchi kwa kuweza kuwapatia vyandarua ambavyo vitawasaidia kujikinga na maambukizi ya ugonjwa wa malaria.
Baadhi ya wananchi kutoka Wilaya ya Kasulu wameipongeza serikali kwa kuwapatia vyandarua hivyo na kuhimizana kuvitumia kwa lengo lililokusudiwa.
Kampeni hiyo ni sehemu ya juhudi za serikali kupunguza maambukizi ya malaria nchini kwa kuhakikisha kila kaya inakuwa na chandarua bora chenye dawa ya kuua mbu.
