Joy FM
Joy FM
13 March 2026, 14:01

Zana za kilimo ni vifaa vinavyotumika kurahisisha shughuli za kilimo kama kulima, kupanda, kupalilia na kuvuna na zina umuhimu mkubwa kwa wananchi hasa wanaotegemea kilimo kama chanzo cha maisha.
Na Mwandishi wetu
Wananchi wa Kijiji cha Nyanganga, Kata ya Kazuramimba, Wilayani Uvinza Mkoani Kigoma wameishukuru Serikali kwa kuona umuhimu wa kuwainua wakulima kupitia uzinduzi wa Kituo cha Zana za Kilimo kitakachosaidia kupunguza utegemezi wa jembe la mkono.
Akizungumza katika kikao na wananchi wa kijiji hicho, Mkuu wa Wilaya ya Uvinza, Mh. Dinah Mathamani, amesema Serikali imeanzisha kituo hicho kwa lengo la kurahisisha shughuli za kilimo kwa wakulima ili waweze kulima maeneo makubwa zaidi na kuongeza uzalishaji.

Mh. Dinah ameeleza kuwa tayari Serikali imeleta power tiller (pawatila) ambayo itatumika kuwasaidia wakulima katika shughuli za maandalizi ya mashamba kuelekea msimu wa kilimo, hatua itakayochochea kilimo cha kisasa na chenye tija kwa wananchi.
Kwa upande wake, Katibu Tawala wa Wilaya ya Uvinza, Ndg. James Mkumbo, amewahimiza wananchi kutumia fursa hiyo vizuri kwa kulima kilimo chenye tija kitakachosaidia kuinua uchumi wa familia na jamii kwa ujumla.

Naye Diwani wa Kata ya Kazuramimba, Mh. Mussa Chessa, kwa niaba ya wananchi wa kata hiyo ameishukuru Serikali kwa kuthamini juhudi za wakulima wa eneo hilo na kuanzisha kituo hicho, akieleza kuwa kitasaidia kuongeza uzalishaji wa mazao na kuboresha maisha ya wananchi.
Mh. Musa amesema wananchi wa kata hiyo wataendelea kushirikiana na Serikali kuhakikisha kituo hicho kinatumika ipasavyo kwa manufaa ya wakulima na maendeleo ya jamii.