Joy FM
Joy FM
10 March 2026, 16:37

Shirika la Posta Tanzania limesema litaendelea kuunga mkono juhudi za serikali katika kuboresha miundombinu ya elimu kwa lengo la kuinua taaluma kwa wanafunzi kwa kuhakikisha wanafunzi wanajifunza katika mazingira rafiki.
Na Hagai Ruyagila
Mkuu wa wilaya ya Kasulu Mkoani Kigoma Kanali Isaac Mwakisu, amekabidhi madawati 100 yenye thamani ya shilingi milioni 8 katika shule ya Msingi Kigondo yaliyotolewa na shirika la Posta Tanzania kwa lengo la kupunguza changamoto ya upungufu wa madawati shuleni hapo.
Akizungumza katika hafla ya Kukabidhi madawati hayo, Kanali Mwakisu akiwa ni mgeni rasmi amelishukuru shirika la Posta Tanzania kwa msaada huo.

Pia amewataka wanafunzi pamoja na walimu wa shule hiyo kuhakikisha wanayatunza madawati hayo ili yaweze kudumu kwa muda mrefu na kuwasaidia wanafunzi wengi zaidi kunufaika nayo.

Kwa upande wake, Mwakilishi wa Postamasta Mkuu wa Tanzania, Ferdinand Kabyemela amewataka wanafunzi wa shule ya msingi Kigondo kusoma kwa bidii ili waweze kufikia ndoto zao na kuwa mchango chanya kwa jamii na Taifa kwa ujumla.

Mwalimu mkuu wa shule ya Msingi Kigondo Mwalimu, Adamu Masendeka amelishukuru Shirika la Posta Tanzania kwa msaada huo wa madawati. ambapo amesema msaada huo utasaidia kuboresha mazingira ya kujifunzia kwa wanafunzi na kupunguza changamoto ya uhaba wa madawati uliyokuwa ukiikabili shule hiyo.
