Joy FM
Joy FM
27 February 2026, 17:22

Katika dunia ya leo yenye ushindani mkubwa wa kiuchumi, vijana wanahitaji maarifa na ujuzi utakaowawezesha kujitegemea na kukabiliana na changamoto za maisha na mojawapo ya elimu muhimu wanayopaswa kupewa ni elimu ya biashara ili iweze kuwasaidia kuelewa misingi ya ujasiriamali, usimamizi wa fedha, na namna ya kuendesha shughuli za kiuchumi kwa ufanisi.
Na Mwandishi wetu
Vijana wilayani Kibondo mkoani Kigoma wametakiwa kuunda vikundi ambavyo vitawawezesha kupata mikopo kutoka halmashari kupitia mapato ya ndani
Hayo yameelezwa na Afisa maendeleo ya jamii na Afisa vijana wa Halmashauri hiyo Bw. Paschal Msoffe wakati akiongea na vijana kupitia mafunzo ya biashara kwa vijana 50, mafunzo ambayo yamefanyika katika ukumbi wa kanisa la Anglikana mjini Kibondo.
Msoffe amesema ili kijana aweze kufanikiwa, anapaswa kuanza biashara katika mtaji alionao, kushirikisha vijana wengine pamoja na kujiunga katika vikundi vya ujasiriamali

Mmoja wa wawezeshaji katika mafunzo hayo Bi. Anita Bosco Joel amesema mafunzo hayo yamefanyika kwa siku 7 lengo likiwa ni kuwajengea uwezo vijana namna ya kuanzisha biashara na mafunzo yametolewa kwa ushirikiano wa halmashauri ya wilaya ya Kibondo pamoja na shirika la Enabel kupitia mradi wa wezesha binti.
Amesema mafunzo yanatolewa kila mwezi katika halmashauri zote za mkoa wa Kigoma na kwa mafunzo ya wilayani Kibondo kwa mwezi Februari vijana 50 ambao asilimia 80 ni (KE) na asilimia 20 (me) wamepatika kupitia matangazo ya makanisani, sokoni na makundi ya Whats App
Baadhi ya vijana ambao wamepata mafunzo hayo ambao ni Dorice James, Obadia Nestory, Faraja Gabriel na Jafari Magulu wamesema mafunzo hayo yatawasaidia katika kuanzisha na kuendeleza biashara.
Hata hivyo afisa maendeleo ya jamii na afisa vijana wa halmashauri iyo Bw. Paschal Msoffe amesema halmashauri imekuwa ikikamilisha malengo ambayo mashirika yanaanzisha na kuwekeza kwa vijana kwa kuwapatia mikopo na kufuatilia ustawi wa vijana hao katika shughuli wanazozifanya.