Joy FM
Joy FM
17 February 2026, 10:51

Mamlaka ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira Kasulu Mjini (KUWASA) imesema inaendelea kuboresha upatikanaji wa huduma ya maji kwa wananchi ili kuhakikisha wanapata maji safi na salama kwa matumizi ya kila siku.
Akizungumza kuhusu hali ya huduma hiyo, Kaimu Mkurugenzi wa KUWASA, Mhandisi Samweli Kayombo, amesema hadi sasa kiwango cha upatikanaji wa maji katika Mji wa Kasulu kimefikia asilimia 71. Ameeleza kuwa hatua hiyo ni matokeo ya jitihada zinazoendelea za serikali katika kuimarisha huduma za kijamii.
Mhandisi Kayombo amesema mamlaka hiyo inaendelea na ujenzi na uboreshaji wa miundombinu ya maji katika maeneo mbalimbali ya halmashauri ili kupunguza changamoto ya upatikanaji wa maji inayowakabili baadhi ya wananchi.
Kwa upande wao, baadhi ya wananchi wa Halmashauri ya Mji Kasulu wamepongeza juhudi zinazofanywa na KUWASA, wakisema kumekuwa na maboresho ya huduma ya maji ikilinganishwa na miaka iliyopita, ingawa bado wanaiomba mamlaka hiyo kuongeza kasi ya usambazaji wa maji katika maeneo ambayo hayajafikiwa kikamilifu.