Joy FM

ENABEL yakabidhi vifaa kwa vijana wanaoishi mazingira magumu Kigoma

27 January 2026, 08:04

Mkuu wa Mkoa Kigoma akipokea vifaa kutoka ENABEL kwa ajili ya vijana wanaoishi mazingira magumu, Picha na Ofisi ya mawasiliani Kigoma

Wadau mbalimbali wa maendeleo Mkoani Kigoma wametakiwa kuendelea kijitokeza na kuwasaidia vijana wanaoishi katika mazingira magumu ili waweze kufikia ndoto zao

Na Mwandishi wetu

Shirika la Maendeleo la watu wa Ubelgiji (Enabel) kupitia Programu ya wezesha binti, limekabidhi vifaa mbalimbali vyenye Thamani ya Shilingi Mil. 794 kwa vijana wanaoishi katika mazingira magumu na washindi kitaalum katika halmshauri tano za mkoa wa Kigoma.

Mkuu wa Mkoa Kigoma akipokea baiskeli ilitolewa na ENABEL kwa ajili ya vijana, Picha na Ofisi ya mawasiliano

Vifaa vilivyokabidhiwa ni pamoja na Matenti 13, baiskeli 270, vifaa vya michezo pamoja na madaftari kwa wanufaika hao katika halmashauri za Kigoma Ujiji, Wilaya ya Kigoma, Halmashauri ya mji na Wilaya Kasulu  pamoja na Kibondo.

Mara baada ya kupokea vifaa hivyo kutoka kwa mfadhili huyo na kuvikabidhi kwa Wakuu wa Wilaya katika maeneo lengwa, Mkuu wa Mkoa wa Kigoma Balozi Simon Sirro anasema mradi wa wezesha binti  umekuwa na mchango mkubwa katika kukuza elimu jumuishi kwa kuwagusa watoto wanaoishi katika mazingira magumu.

Mkuu wa Mkoa Kigoma Balozi Simon Sirro akiwa kwenye picha na viongozi wa ENABEL na wengine kutoka serikalini, Picha na Ofisi ya mawasiliano Kigoma

Amesema vifaa hivyo vitapunguza utoro na kuimarisha mazingira ya kujifunza na kujifunzia hususani kwa watoto wa kike na kuongeza fursa ya kuzifikia ndoto zao za kielimu.

Mkuu wa Mkoa Kigoma akipokea vifaa vya vijana vilivyotolewa na ENABEL, Picha na Ofisi ya mawasiliano Kigoma

Vifaa hivyo ikiwemo matenti yametolewa kwa ajili ya kuwapatia faragha watoto wa kike katika mazingira ya shuleni, baiskeli kwa ajili ya kurahisisha usafiri kwa wanafunzi wanaoishi makazi yaliyo mbali na shule, pamoja na vifaa vya michezo vyenye lengo la kuimarisha afya, ushirikiano na kujiamini.