Joy FM

TMDA yatakiwa kusimamia ubora na udhibiti wa bidhaa za kiafya Kigoma

17 December 2025, 07:59

Mkuu wa Mkoa Kigoma Balozi Simon Sirro akiwa na Meneja wa TMDA ofisini wakizungumzia udhibiti wa dawa zisizofaa, Picha na Ofisi ya mawasiliano

Mamlaka ya usimamizi wa chakula na vifaa tiba Tanzania TMDA Kanda ya Magharibi imesema itaendelea kufanya operesheni mbalimbali kwa ajili ya kudhibiti bidhaa za afya zinazoingizwa nchi kinyuma cha sheria na ambazo hazikidhi vigezo

Na Mwandishi wetu

Mkuu wa Mkoa wa Kigoma Balozi Simon Sirro ameutaka uongozi wa Mamlaka ya Usimamizi wa Chakula na Vifaa Tiba Tanzania (TMDA) Kanda ya Magharibi, kuongeza kasi katika kusimamia ubora na udhititi bidhaa za kiafya ili kulinda afya za wakazi kutokana na mkoa kupakana na nchi jirani, jambo linaloweza kutoa mianya kwa wafanyabiashara wasio waaminifu kuingiza bidhaa tiba mkoani hapa bila kuzingatia sheria na taratibu za nchi.

Balozi Sirro amesema hayo alipokutana na kufanya mazungumzo na uongozi wa TMDA, ofisini kwake leo Desemba 16, 2025 na kusisitiza kuwa, usimamizi na ufuatiliaji wa karibu unatakiwa kuzidi kufanyika ili kubaini dawa feki na bidhaa za kiafya qzisizo na viwango zinazoingizwa nchini kinyume na sheria kabla ya kuleta athari kwa watumiaji wa mwisho.

Baadhi ya watumishi wa TMDA wakiwa ofisi ya Mkuu wa Mkoa Kigoma wakiteta jambo na Mkuu wa Mkoa Kigoma Balozi Simon Sirro, Picha na Ofisi ya Mawasiliano Kigoma

Ameipongeza mamlaka  hiyo kwa kazi nzuri inayoifanya katika kuendelea kusimamia uzalishaji wa bidhaa za kiafya na chakula kwani utimamu wa Afya za wananchi ni kichocheo kikubwa cha Maendeleo ya mkoa na taifa kwa ujumla.

Meneja wa TMDA Kanda ya Magharibi Christopha Osward amesema, mamlaka hiyo inaendelea kufanya ukaguzi wa mara kwa mara katika maduka ya dawa,  vituo vya Afya, Hospitali pamoja na kutoa Elimu kwa wadau wa Afya kuhusu utambuzi na matumizi sahihi ya vifaa tiba na dawa.

Meneja wa TMDA Kanda ya Magharibi Christopha Osward na timu yake wakizungumza na Mkuu wa Mkoa wa Kigoma Balozi Simon Sirro, Picha na Ofisi ya mawasiliano Kigoma

Amesema mamlaka itaendelea kushirikiana na wataalam wa Afya ngazi ya mkoa na mamlaka za Serikali za mitaa katika kuhakikisha wanatoa huduma bora na yenye kukidhi viwango vya utoaji wa huduma kwa jamii.