Joy FM

Wahitimu TIA Kigoma waaswa kuwa wabunifu katika biashara

22 November 2025, 09:31

Mkuu wa Mkoa wa Kigoma akiwa na viongozi wengine wakiwa wamevalia majoho tayari kwa mahafali ya wahitimu TIA, Picha na Ofisi ya mawasiliano Kigoma

Wahitimu wa fani mbalimbali katika chuo cha uhasibu ndaki ya Kigoma wametakiwa kuendelea kuwa wabunifu ili waweze kujiajiri na kuacha kuendelea kusubiri kuajiriwa na serikali au mashirika binafsi.

Na Mwandishi wetu

Mkuu wa Mkoa Kigoma Balozi Simon Sirro amewataka wahitimu wa kozi mbalimbali katika Taasisi ya  Uhasibu Tanzania (TIA) Kampasi ya Kigoma, kutumia elimu waliyopata kuisaidia jamii mkoani hapa katika kufanya ubunifu na kusambaza ujuzi wa  usimamizi wa biashara ili  shughuli za kiuchumi zinazofanyika ziwe na tija kubwa.

Sirro amesema hayo wakati wa mahafali ya 23 ya TIA Kampasi ya Kigoma yaliyofanyika katika majengo mapya ya Kampasi hiyo yaliyo eneo la Kamara Kata ya Mngonya Halmashauri ya wilaya Kigoma mkoani Kigoma, ambapo jumla ya wahitimu 756 wametunukiwa cheti cha awali na Diploma katika kozi mbalimbali za uhasibu, usimamizi wa rasilimali watu, ugavi na manunuzi.

Wahitimu wa fani mbalimbali chuo cha TIA ndaki ya Kigoma wakiwa kwenye mahafali, Picha na Ofisi ya mawasiliano Kigoma

Mkuu huyo wa Mkoa Kigoma alisema kuwa kuwa, muhitimu haina maana ya kupata cheti lakini cheti hicho kitakuwa na thamani kama elimu iliyopatikana itatumika kuisaidia jamii hasa watu wa kipato cha chini walio wengi kufanya shughuli zao kwa tija na kuweza kuinua kipato chao.

Kwa upande wake, Katibu Tawala wa mkoa Kigoma,Hassan Rugwa amesema kuwa elimu ya biashara ni  msingi mkubwa wa shughuli za binadamu kwani huwaunganisha wenye kipato kikubwa na kidogo katika kuendesha maisha.

Katibu tawala Mkoa wa Kigoma Hassan Rugwa akizungumza wakati wa mahafali ya chuo cha TIA, Picha na Ofisi ya mawasikiano Kigoma

Akitoa taarifa kuhusiana na mahafali hayo, Mtendaji Mkuu wa TIA, Prof. William Pallangyo alisema kuwa jumla ya wahitimu 756 wametunukiwa vyeti mbalimbali ambapo kati yao wahitimu wa cheti cha awali 262 ,Astashahada wakiwa 251 na Stashahada wapo 243.