Joy FM
Joy FM
17 November 2025, 13:24

Wazazi na walezi Mkoani Kigoma wametakiwa kuhakikisha wanawalea watoto wao katika malezi yaliyo bora
Na Hagai Ruyagila
Katibu tawala wa mkoa wa Kigoma Hassan Rugwa amewataka maafisa maendeleo ya jamii na maafisa ustawi wa jamii katika Halmashauri zote za Mkoa huo kuendelea kutoa elimu ya malezi kwa jamii ili wazazi na walezi waweze kuwalea watoto wao kwa njia bora hatua itakayochangia katika ukuaji mzuri wa watoto.
Rugwa amesema hayo katika kikao kazi cha mafunzo ya wawezeshaji wa vikundi vya malezi na matunzo ya watoto kilichohusisha halmashauri zote za mkoa wa Kigoma ambacho kimefanyika Mjini Kasulu.
Amesema ukuaji bora wa mtoto unategemea malezi bora, lishe sahihi pamoja na kuzingatia maadili mema kutoka kwa wazazi na walezi.
Afisa maendeleo ya jamii mkoa wa Kigoma Msafiri Nzunuri amesema changamoto nyingi zinazowakumba watoto zanatokana na wazazi na walezi kutozingatia majukumu yao ipasavyo, jambo ambalo linalosababisha baadhi ya watoto kupata mimba katika umri mdogo, na hatimaye kuacha masomo.
Amesema serikali itaendelea kutoa mafunzo ya malezi ili kukabiliana na changamoto hizo.

Afisa meendeleo ya Jamii Mkuu kutoka Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Makundi Maalum, Vaileth Mulyalya amesema wizara imeandaa sera ya malezi na imeahidi kuanzisha vikundi vya malezi inchi nzima ili kuimarisha ustawi wa watoto.

Mtaalamu kutoka UNICEF kutoka kitengo cha ulinzi wa mtoto Juliana Karusha amesema elimu ya malezi inayotolewa na maafisa maendeleo ya jamii imechangia kuongeza ufaulu wa wanafunzi na kukuza taaluma mashuleni.
Akizungumza kwa niaba ya washiriki wa mafunzo hayo Mustafa Mtungwe, ambaye ni mwakilishi wa Maafisa Maendeleo ya Jamii na Maafisa Ustawi wa Jamii amesema mafunzo hayo yamewajengea uwezo zaidi yakuendelea kutoa elimu sahihi ya malezi na ulinzi wa mtoto kwa jamii.