Joy FM

Zaidi ya wananchi 3500 kupatiwa huduma za kibingwa Kigoma

11 October 2025, 16:30

Daktari bingwa ambaye pia ni Mganga Mfawidhi Hospitali ya rufaa Maweni, Picha na Orida Sayon

Katika kuadhimisha miaka 53 tangu kuanzishwa kwa Hospitali ya rufaa ya Mkoa wa Kigoma Maweni, Hospitali hiyo inatarajia kutoa huduma za matibabu ya kibingwa kwa wananchi wa Mkoa wa Kigoma kuanzia jumatatu ya Oktoba 13 hadi 17 mwaka huu wa 2025

Na Orida Sayon

Zaidi ya wananchi 3500 kutoka maeneo mbalimbali ya Mko wa Kigoma na meneo jirani wanatarajia kupatiwa huduma za matibabu ya kibingwa ambazo zinatarajiwa kutolewa na madaktari bingwa na bingwa bobezi katika Hospitali ya rufaa ya Mkoa wa Kigoma Maweni.

Akizungumza na waandishi wa habari, Daktari bingwa na Kaimu Mganga Mfawidhi Hospitali ya rufaa ya Mkoa wa Kigoma Maweni Dkt. Joseph Emmanuel Nangawe amesema huduma hizo za kibingwa zinatarajiwa kutolewa kwa wananchi na madaktari bingwa na bingwa bobezi zaidi ya 25 kutoka kada mbalimbali za afya na kada zaidi ya 15 zitakuwa na wataalamu.

Muonekano wa mashine ya Endoscopic UNIT kwa ajili ya uchunguzi wa mfumo chakula, Picha na Orida Sayon

Amesema kambi hiyo inatarajiwa kuanza Oktoba 13 -17 mwa huu wa 2025 katika hospitali ya rufaa ya maweni ikilenga kutoa huduma za kibingwa kwa wananchi wenye shida mbalimbali wa Mkoa wa Kigoma na Mikoa ya jirani.

Sauti ya Kaimu Mganga Mfawidhi wa hospitali ya rufaa ya Mkoa wa Kigoma maweni Dkt. Joseph Emmanuel Nangawe

Aidha Dkt. Joseph Emmanuel Nangawe amehimiza wananchi wenye changamoto za kiafya kujitokeza kwa wingi ili waweze kupata huduma kutoka kwa madaktari bingwa na mabingwa bobezi zilizosogezwa karibu yao ili kuepuka gharama za rufaa ya kwenda mikoa ya nje ya  Kigoma  ikiwemo Mwanza, Dodoma na Dar es salaam.

Mashine ya Mamograph inayotumika kupima mabadiliko ya awali ya Saratani ya titi, Picha na Orida Sayon

Naye Daktari bingwa wa upasuaji wa magonjwa ya mfumo wa mkojo na uzazi kwa wanaume Boniface Kilangi ambaye pia ni mratibu wa huduma za kibingwa Hospitali ya rufaa ya Mkoa wa Kigoma Maweni amesema ujio wa madaktari bingwa unatarajia kuzindua pia huduma mpya za uchunguzi wa mfumo wa chakula itakayotoa huduma kwa wenye changamoto ya magonjwa ya ndani ya tumbo.

Sauti ya Daktari bingwa wa upasuaji wa magonjwa ya mfumo wa mkojo na uzazi kwa wanaume Boniface Kilangi

Kwa upande wake, Dkt. Ashraf Idd Bitalio Mwenyekiti wa kamati ya maandalizi ya kambi ya kibingwa Hospitali ya rufaa ya Mkoa wa Kigoma Maweni amesema kambi hiyo itaongeza wigo wa utoaji huduma huku huduma hizo zitahusisha wenye bima, wasio na bima na watu wenye kipato cha chini watapata nafasi ya kutibiwa kulingana na utaratibu utakaowekwa.

Sauti ya Dkt. Ashraf Bitalio Mwenyekiti wa kamati ya maandalizi ya kambi ya kibingwa Hospitali ya rufaa ya Mkoa wa Kigoma Maweni

Ujio wa madaktari bingwa na bingwa bobezi katika Hospitali ya rufaa ya Mkoa wa Kigoma Maweni utaenda sambamba na maadhimisho ya miaka 53 tangu kuanzishwa kwa hospitali ya maweni ambayo ilianzishwa mnamo mwaka 1972 na imeendelea kutoa huduma bora kwa wananchi wa Kigoma na maeneo ya jirani.

Muonekano w mashine ya CT Scan kwa ajili ya uchunguzi wa magoinjwa mblimbali ya mwili, Picha na Orida Sayon