Joy FM
Joy FM
17 September 2025, 09:11

Mwenge wa uhuru umeendelea kukimbizwa katika Halmashauri za Mkoa wa Kigoma kwa kutembelea na kuweka mawe ya msingi
Na Hagai Ruyagila
Miradi mbalimbali ya maendeleo ikiwemo miradi ya shule afya na miradi ya vikundi vya vijana na wanawake katika Halmashauri ya Mji wa Kasulu mkoani Kigoma inatarajiwa kutembelewa, kukaguliwa, na kuzinduliwa na Mwenge wa Uhuru kwa mwaka 2025.
Hayo yameelezwa na Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya Mji Kasulu Mwl. Vumilia Simbeye wakati akizungumza na vyombo vya habari na kueleza kuwa maandalizi yote muhimu yamekamilika kwa kwa kiasi kikubwa na kwamba halmashauri hiyo ipo tayari kwa ajili ya kuupokea Mwenge wa Uhuru kuanza mbio zake katika halmashauri hiyo.
Aidha Mwl, Simbeye ametoa wito kwa wananchi kujitokeza kwa wingi kuupokea Mwenge wa Uhuru kuonesha mshikamano, uzalendo na kuunga mkono juhudi za maendeleo zinazotekelezwa katika maeneo ya wananchi.
Baadhi ya wananchi wa halmshauri ya mji wa Kasulu wameeleza furaha yao kuhusu ujio wa Mwenge wa Uhuru, wakisema kuwa ni fursa ya kipekee kuona miradi ya maendeleo inayotekelezwa katika maeneo yao ikikaguliwa na kuthibitishwa na viongozi wa kitaifa ili iweze kutoa huduma na kutatua changamoto zao.
Mbio za Mwenge wa uhuru zinatarajiwa kukimbizwa katika halmashauri ya mji wa Kasulu Septemba 18 mwaka huu ikiwa na kauli mbiu isemayo “jitokeze kushiriki uchaguzi Mkuu wa mwaka 2025 kwa Amani na Utulivu”.