Joy FM
Joy FM
1 September 2025, 14:50

Wananchi wa Mtaa wa Butunga Relini Manispaa ya Kigoma Ujiji wameeleza kushamiri kwa matukio ya mauaji ya watu na kuomba ulinzi uimarishwe kwani hilo ni tukio la tatu ndani ya kipindi kifupi.
Na Josephine Kiravu
Mtu mmoja ambaye hajatambulika mara moja jina lake amekutwa akiwa ameuawa kwa kukatwakatwa na mapanga katika maeneo mbalimbali ya mwili wake katika mtaa wa Butunga kata ya Kibirizi Manispaa ya Kigoma Ujiji.
Akithibitisha kutokea kwa tukio hilo, Mwenyekiti wa Mtaa wa Butunga Hamisi Yasin amesema kwa mujibu wa baadhi ya mashuhuda wa tukio hilo, mtu huyo ni mkazi wa mtaa wa Mlole huku akieleza tukio kuwa la kinyama.
Na hapa anatoa wito kwa serikali kuhakikisha wanawasaka waliohusika na tukio hilo sambamba na kusambaratisha makundi ya vijana wanaojiuhusisha na uvutaji wa bangi na uchezaji wa kamari kwani mara kadhaa vijana hao wamekuwa wakitajwa kuhusika kwenye matukio ya uhalifu.
Kwa upande wake, Kamanda wa Polisi mkoani Kigoma SACP Filemon Makungu amekiri kuwepo kwa tukio hilo na kwamba tayari ndugu wa marehemu wamekabidhiwa mwili na uchunguzi unaendelea ili kubaini chanzo cha tukio hilo.