Joy FM

CRS yatoa elimu ya kubadili taka kuwa fursa

4 July 2025, 16:05

Muonekano wa taka ambazo zinatajwa kuwa fursa kwa wafanyabiashara, Picha na Mtandaoni

Kubadili taka kuwa fursa ni mchakato wa ubunifu unaohusisha matumizi ya maarifa, teknolojia na ujasiriamali ili kutumia taka kama rasilimali yenye thamani badala ya kuona taka kama uchafu.

Na Josephine Kiravu

Zaidi ya wafanyabiashara 250 na wadau mbalimbali wa mazingira na uchumi Mkoani Kigoma wamepatiwa mafunzo ya namna ya kubadili taka na kuwa fursa sambamba na kulinda maji ya Ziwa Tanganyika.

Wafanyabiashara hao pamoja na wadau mbalimbali wamekutana kwa lengo la kupata mafunzo ambayo yameandaliwa shirika la CRS kwa kushirikiana na CARITAS pamoja na TCCIA chini ya mradi wa The Voices.

Wafanyabiashara na wadau wa mazingira wakiwa katika semina iliyoandaliwa na CRS, Picha na Josephine Kiravu

Meneja mradi wa The Voices Robert Adrian amesema lengo la mafunzo hayo ni kubadili taka kuwa fursa pamoja na kutunza maji ya ziwa Tanganyika kwa kuzuia uchafuzi wa mazingira na kutumia vyema dampo la msimba kwenye ukusanyaji wa taka.

Sauti ya Meneja mradi wa The Voices Robert Adrian

Kwa upande wake, Katibu wa Chemba ya biashara mkoani Kigoma (TCCIA) Prosper Guga amesema changamoto kubwa inayowakabili wajasiriamali ni elimu hivyo kupitia mafunzo hayo yatasaidia kuwafungua na kutumia taka kama fursa.

Sauti ya Katibu wa Chemba ya biashara Mkoani Kigoma (TCCIA) Prosper Guga

Nao baadhi ya wadau waliohudhuria katika mafunzo hayo akiwemo Genoviva Mtiti wamesema awali taka hizo ikiwemo chupa za maji zilionekana kama uchafu lakini kupitia elimu waliyoipata itasaidia kwa kiasi kikubwa wajasiriamali na wafanyabiashara kuchukulia kama fursa kwao.

Sauti ya baadhi ya wadau wa mazingira na biashara

Kwa mujibu wa meneja mradi wa The Voice tayari imetengwa ruzuku kwa ajili ya kuwawezesha wajasiriamali na wafanyabisahara huku akizitaka pia taasis za fedha kufungua milango ya mikopo ili kuwawezesha kuendesha shughuli zao.