Joy FM
Joy FM
4 June 2025, 12:15

Watoto wenye mahitaji maalum wamepewa sare za shule wilayani Kasulu.
Na Hagai Ruyagila
Wadau wa maendeleo katika Wilaya ya Kasulu mkoani Kigoma wametakiwa kuendelea kujitokeza kuwasaidia wanafunzi wenye mahitaji maalumu, hususan wale wenye ulemavu wa viungo, ili kuwawezesha kutimiza ndoto zao za kielimu na maisha kwa ujumla.
Wito huo umetolewa na mdau wa sekta ya elimu, Mwalimu Yusuph Ibrahimu kutoka Shule ya Msingi Kisuma, iliyopo katika Halmashauri ya Wilaya ya Kasulu, baada ya kutoa msaada sare za shule kwa wanafunzi 35 wenye mahitaji maalum katika Shule ya Msingi Kalema.

Amesema watoto wenye mahitaji maalumu wanahaki kama watoto wengine hivyo wanapaswa kusaidiwa ili kuiunga mkono serikali ya awamu ya sita ambayo imekuwa ikitoa elimu bure kwa wanafunzi hapa nchini.
Kaimu Mwalimu mkuu wa Elimu Maalum katika Shule ya Msingi Kalema, Bi. Merry Amon, amempongeza Mwalimu Yusuph kwa moyo wake wa huruma na kujitoa kusaidia watoto wenye uhitaji.
Naye Mkurugenzi wa Taasisi ya Usilie Tena kutoka jijini Dar es Salaam, Bi. Egra Kamugisha, ameahidi kuwakabidhi watoto hao kadi za bima ya afya bure, ili kuwasaidia wanapopata changamoto za kiafya.
Mmoja wa wanafunzi wenye mahitaji maalum kutoka Shule ya Msingi Kalema, amemshukuru mdau huyo wa elimu kwa msaada huo na kuahidi kusoma kwa bidii ili kufanikisha malengo yake.
Kituo cha watoto wenye mahitaji maalum katika Shule ya Msingi Kalema, kilichopo Halmashauri ya Mji Kasulu, kwa sasa kinahudumia jumla ya watoto 40. Msaada unaotolewa na wadau mbalimbali unaendelea kuwa chachu muhimu katika kuhakikisha watoto hao wanapata mazingira bora ya kujifunza na kuishi.