Joy FM
Joy FM
16 May 2025, 15:49

Wakulima wilayani Kasulu mkoani Kigoma wametakiwa kuwa na desturi ya kuweka akiba ya chakula ili kukabiliana na njaa.
Na Hagai Ruyagila
Mkuu wa wilaya ya kasulu kanali Isaac Mwakisu amewaagiza Madiwani wa halmashauri ya wilaya ya Kasulu mkoani Kigoma kutoa elimu kwa wananchi kuhusu madhara ya kuuza mazao ya chakula kiholela badala yake wahifadhi kwa ajili ya matumizi ya baadaye ili kukabiliana na changamoto ya uhaba wa chakula katika familia.
Akitoa salamu za serikali katika kikao cha baraza la madiwani cha robo ya tatu halmashauri ya wilaya ya Kasulu Mwaka wa fedha 2024/2025 Mkuu wa wilaya ya Kasulu kanali Isaac mwakisu amesema usalama wa chakula unazidi kushuka kutokana na wananchi wengi kuuza mazao kiholela.
Aidha Kanal Mwakisu amesema huenda wilaya hiyo ikakumbwa na njaa kufuatia wananchi kushindwa kutunza mazao ya chakula hali ambayo inahatarisha zaidi usalama wa chakula na kwamba familia zinatakiwa kuwa makini zaidi katika uuzaji wa mazao hayo ya chakula.
Kwa upande wao Baadhi ya Madiwani kutoka katika halmashauri hiyo wamesema dalili za uhaba wa chakula katika kata zao zimeanza kuonekana kutokana na msururu wa malori yakiendelea kuonekana yakibeba mazao ya wananchi licha ya kuahidi kuendelea kutoa Elimu.

Baadhi ya wakulima wanasema wanauza chakula kwa lengo la kurejesha fedha walizokopa kabla ya kuanza kulima.