Joy FM

Shughuli za uvuvi zafunguliwa rasmi ziwa Tanganyika

16 August 2024, 11:09

Waziri wa uvuvi akikata utepe wakati akizindua shughuli za uvuvi ndani ya ziwa tanganyika, Picha na Kadislaus Ezekiel

Serikali imewataka wavuvi wa samaki ndani ya ziwa tanganyika kuacha uvuvi haramu kwa ajili ya uendelevu vsamaki na dagaa.

Na Kadislaus Ezekiel – Kigoma

Sauti ya ripoti ya mwandishi wetu Kadislaus Ezekiel

Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Abdallah Ulega amezindua zoezi la uvuvi katika  Ziwa Tanganyika baada ya kupumzishwa kwa shughuli za uvuvi katika ziwa hilo  kwa muda wa miezi mitatu. 

Waziri Ulega amezindua zoezi hilo katika Mwalo wa Katonga manispaa ya Kigoma Ujiji  Mkoani Kigoma Agosti 15,2024 na kubainisha kuwa kupumzishwa kwa shughuli za uvuvi kwa miezi mitatu kuanzia Mei 15 hadi Agosti 15 mwaka huu kulikuwa kunalenga kulinda rasilimali za uvuvi kwenye ziwa hilo.

Amesema uamuzi huo wa kupumzisha ziwa ni utekelezaji wa Mkataba wa Kikanda wa Nchi Wanachama wa Mamlaka ya Ziwa Tanganyika (LTA) Unaoweka Hatua za Usimamizi wa Uvuvi Endelevu katika Ziwa Tanganyika na Bonde lake. 

Baadhi ya vifaa vya wavuvi ziwa tanganyika vikiwa tayari kwa ajili yashughuli za uvuvi, Picha na Orida Sayon

Aidha, Waziri Ulega ametumia  jukwaa hilo kuwaelekeza wavuvi kuwa kufunguliwa kwa shughuli za uvuvi kuendane na matumizi sahihi ya zana na njia halali zinazokubalika kisheria ili samaki walioachwa wazaliane na kuemdelea kupatikana kwa muda mrefu  zaidi. 

Akizungumza katika zoezi hilo Naibu Katibu Mkuu wizara ya mifugo na Uvuvi, Dk.Edwin Mhede alisema kuwa uvuvi imekuwa moja ya sekta kuu ya uchumi nchini ikiajiri watanzania milioni sita  Sawa na asilimia 10 ya Watanzania wote.