Joy FM

DC Kigoma azitaka NGO’s kuzingatia maadili ya kitanzania

4 July 2024, 10:12

Mkuu wa wilaya kigoma Mh. Salum Kalli akiwa katika mkutano wa mashirika yasiyo ya kiserikali, Picha na Josephine Kiravu

Wakati mashirika yasiyokuwa ya serikali yakiendelea kuunga mkono juhudi za serikali katika kuleta maendeleo kwa wananchi kwa kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo yametakiwa kutokubali kutumia vibaya kwa lengo la kuchafua taswira ya nchi na kuharibu maadili.

Na Josephine Kiravu – Kigoma

Mkuu wa Wilaya ya Kigoma Ndugu. Salum Hamis  Kali amewataka Viongozi wa Mashirika yasiyo ya Kiserikali kufanya kazi Wilayani hapo kwa kuzingatia misingi, uzalendo na maadili ya Kitanzania.

Ameyasema hayo July 03, 2024 Katika Kikao kazi cha Siku Moja kilichofanyikia ukumbi wa Redcross Manispaa ya Kigoma/Ujiji chenye lengo la Mashirika kuwasilisha Mipango kazi kwa Mwaka mpya wa fedha 2024/2025.

Amesema mashirika yasiyo ya Kiserikali ni wadau mhimu wa Maendeleo katika kufanya kazi ni lazima wahakikishe wanalinda jamii ya Kitanzania  kwa kupinga vitendo na viashiria visivyoakisi maadili ya kitanzania. 

Ni Viongozi wa Mashirika yasiyo ya Kiserikali wakiwa kwenye mkutano wa mashirika yasiyokuwa ya kiserikali, Picha na Josephine Kiravu

Aidha kiongozi huyo ameyataka mashirika hayo kupinga vitendo vya ukatili kwa Wanawake na Watoto, kuijengea uwezo jamii juu ya utoaji taarifa katika mamlaka zinazohusika na kuwajengea Wananchi uwezo kiuchumi, elimu na katika masuala ya kiafya. 

Naye Mratibu wa Mashirika Manispaa ya Kigoma Ujiji Bi. Austina Hwago Amesema Wilaya ya Kigoma ina mashirika yasiyo ya Kiserikali yaliyosajiliwa tisini na  nane (98) ambayo yamekuwa yakitekeleza miradi ya  Maendeleo   katika Sekta ya afya, Uchumi, Kilimo, na uvuvi licha ya baadhi ya Mashirika kutotoa taarifa za utekelezaji wao kwa wakati na kutofuata sera za uwazi na Uwajibikaji.

Baadhi ya wadau wa mashirika binafsi wakiwa kwenye kikao, Picha na Josephine Kiravu

Naye Mwakilishi wa Mashirika yasiyo ya Kiserikali Mkoa wa Kigoma na Mjumbe wa Baraza la Mashirika yasiyo ya Kiserikali Taifa (NACONGO) Ndugu. Alex Luoga amewataka Viongozi wa mashirika hayo kuzingatia kanuni na miongozo kwa kutoa taarifa kwa wakati na kuzingatia misingi na maadili ya Taifa.