Joy FM

Wananchi Mwilamvya wachanga milioni 14 kujenga shule mpya

2 July 2024, 08:42

Wananchi wa kata ya Mwilamvya mjini Kasulu wakiwa katika kikao cha kujadili sehemu ya kujenga shule mpya. Picha na Emmanuel Kamangu

Ili kukabiliana na chamgamoto ya watoto kutembea umbali mrefu kwa wananchi wa kata ya Mwilamvya wilayani Kasulu, hatimaye wananchi wamekubaliana kushirikiana na wadau wa maendeleo kuchanga pesa kwa ajili ya kuanza ujenzi wa shule mpya katani hapo.

Na Emmanuel Kamangu – Kasulu

Zaidi ya shilingi milioni 14 zimechangwa na wananchi pamoja na wadau wa maendeleo kata ya Mwilamvya halmashauri ya mji wa kasulu ili kufidia eneo ambalo ni  mashamba ya wananchi  kwa ajili ya kupisha ujenzi mpya  wa shule ya  msingi Mwilamvya. 

Akizungumza katika mkutano wa hadhara Diwani wa kata ya Mwilamvya halmashauri ya mji wa Kasulu Bw. Emmanuel Gamuye ameendelea kuwaomba wananchi kuchangia michango ili kufanikiwa kufidia eneo husika ambalo limependekezwa kujengwa kwa shule mpya ya msingi ikiwa ni kuwanusuru  wanafunzi na adha ya kutembelea umbali mrefu kufuata elimu.

Sauti ya Diwani wa kata ya Mwilamvya halmashauri ya mji wa Kasulu Bw. Emmanuel Gamuye

Kwa upande wake Makamu Mwenyekiti halmashauri ya mji wa Kasulu Bw. Seleman Kwirusha amewasihi wananchi wa kata ya Mwilamvya kuchangamkia fursa hiyo ili kuharakisha maendeleo hasa kwa kuwasaidia watoto wadogo kupata huduma ya elimu karibu.

Sauti ya Makamu mwenyekiti halmashauri ya mji wa Kasulu Bw, Seleman

Aidha wananchi wa kata ya Mwilamvya wakiwa katika mkutano huo wamesema watahakikisha kwa kila namna wanamuunga mkono Diwani Gamuye ili kufika mwakani shule mpya ya msingi Mwilamvya  iwe tayari imekamilika.

Sauti ya wananchi wa kata ya Mwilamvya wakiwa katika mkutano

Hata hivyo wananchi hao wameongeza kuwa kwa mwananchi atakayekaidi kuchangia mchango wa kuanzia elfu tano kama walivyokubaliana  kwa ajili ya ujenzi wa shule mpya ya msingi watamuona kama adui namba moja wa maendeleo ya kata yao.

Baadhi ya viongozi wa kata ya Mwilamvya wakiwa katika mkutano wa hadhara kujadili maendeleo, Picha na Emmanuel Kamangu