Joy FM

FPCT Kigoma yatoa msaada kwa watoto yatima

25 June 2024, 11:54

Ni baadhi ya waumini wa kanisa la FPCT manispaa ya kigoma ujiji, wametoa msaada kwa watoto yatima, Picha na Lucas Hoha

Jamii na wadau wa maendeleo Mkoani Kigoma wameombwa kujitokeza na kuendelea kusaidia watoto yatima wanaolelewa na kituo cha matyazo kilichopo kata ya kalinzi halmashauri ya wilaya kigoma.

Na Lucas Hoha – Kigoma

Kanisa la The Free  Pentekosite Church of Tanzania FPCT Mwanga lililopo Manispaa ya Kigoma  Ujiji kupitia idara ya Vijana Kanisani wametoa msaada wa vitu mbalimbali ikiwemo mafuta, sabuni na sukari vyenye thamani ya zaidi ya shilingi laki tisa katika kituo cha kulea watoto yatima Matyazo kilichopo kata ya kalinzi Halmashauri ya Wilaya ya Kigoma.

Kanisa la FPCT limetoa msaada wa vitu mbalimbali kwa watoto yatima matyazo, Picha na Lucas Hoha

Akizungumza wakati wa kukabidhi vitu hivyo, katibu wa Kanisa la FPCT Mwanga Mchungaji Amon Anania amesema msaada huo  ni sehemu ya wajibu wa kanisa kuihudumia jamii na kutimiza maagizo ya maandiko matakatifu yanayoagiza kuwasaidia watoto yatima.

Sauti ya Katibu wa kanisa la FPCT Mwanga

Kwa upande wake, Mratibu wa idara ya vijana Kanisani  Samwel Yusuph Kidaha mbali na kutoa shukrani kwa  vijana kuchangia msaada huo ametoa wito kwa mashirika na watu binafsi kujitokeza kutoa msaada kwa watoto hao kwani bado wana mahitaji mbalimbali.

Sauti ya Mratibu wa Idara ya vijana

Isac Ngajagu ni Afisa ustawi wa jamii na mlezi wa watoto katika kituo hicho amesema msaada huo ambao umetolewa na kanisa la FPCT Mwanga utasaidia kupunguza baadhi ya gharama kituoni hapo kwani wamekuwa wakitumia zaidi ya shilingi milioni 30 kwa mwezi katika kuwahudumia watoto hao, huku akiongeza kuwa wanatoa msaada kwa watoto waliotelekezwa na wazazi na wale wanaoishi kwenye mazingira hatarishi.

Sauti ya Afisa ustawi wa jamii wa kituo

Nao baadhi ya vijana wa Kanisa la FPCT Mwanga wanaeleza sababu iliyowafanya kutoa msaaa huo.

Sauti ya vijana wa kanisa la FPCT Mwanga manispaa ya kigoma

Kituo cha kulea watoto yatima matyazo kwa sasa kina jumla ya watoto 53 na kiko chini ya Kanisani la Anglikana Dayosisi ya Western Tanganyika na kimekuwa kikipokea watoto wenye mahitaji  kutoka mikoa mbalimbali Tanzania kwa kushirikiana na serikali.