Joy FM
Joy FM
10 April 2026, 14:46

Uboreshwaji wa soko lolote kunachochea ukuaji wa biashara ndogo na za kati, kuongeza ajira, pamoja na kuinua uchumi wa eneo husika.
Na Hagai Ruyagila
Wananchi wa Kata ya Heru Juu, Halmashauri ya Mji Kasulu Mkoani Kigoma, wameiomba serikali kuboresha miundombinu ya soko hilo itakayowawezesha wafanyabiashara kufanya shughuli zao katika mazingira safi, salama na yenye mpangilio mzuri.
Ombi hilo limetolewa na Etira Mafugo wakati wa mkutano wa hadhara ulioongozwa na Diwani wa kata ya Heru Juu, Gilbert Rugali, aliyekuwa akisikiliza na kupokea kero mbali mbali za Wananchi.
Akizungumza katika mkutano huo, Etira Mafugo amesema hali ya sasa siyo ya kuridhisha kutokana na kukosa mpangilio mzuri pamoja na miundombinu muhimu, jambo linalosababisha usumbufu kwa wafanyabiashara na wateja.
Kwa upande wake, Afisa Mtendaji wa Kata ya Heru Juu, Habili Masumay, amesema eneo linalotumika kwa shughuli za biashara halina muonekana na mpangilio unaokidhi mahitaji ya soko bora.

Ameeleza kuwa uongozi wa kata utakaa pamoja na wananchi na wafanyabiashara ili kujadili na kupanga mikakati bora ya kujadili namna gani ya kujenga soko.
Aidha, amesema kuwa watashirikiana kwa karibu na Diwani wa kata hiyo kuhakikisha suala la uboreshaji wa soko linawekwa miongoni mwa vipaumbele vya maendeleo ya kata, kwa lengo la kuinua shughuli za kiuchumi na kuboresha mazingira ya biashara kwa wananchi.