Joy FM

Maafisa usafirishaji wapewa mkopo wa pikipiki Kasulu

27 March 2026, 18:10

Pikipiki zilizokabidhiwa kwa Umoja wa maafisa usafirishaji maarufu kama bodaboda katika Kijiji na Kata ya Makere, Picha na Tryphone Odace

Serikali imeendelea kuwawezesha vijana kupitia mikopo ya asilimia kumi, huku waendesha bodaboda katika Kata ya Makere wilayani Kasulu mkoani Kigoma wakisema hatua hiyo imebadili maisha yao kwa kiasi kikubwa.

Na Mwandishi wetu

Umoja wa maafisa usafirishaji maarufu kama bodaboda katika Kijiji na Kata ya Makere, Halmashauri ya Wilaya ya Kasulu Mkoani Kigoma, wameipongeza Serikali kwa kuwawezesha kupata mikopo ya asilimia kumi, hatua iliyowawezesha kununua pikipiki na kuboresha maisha yao kiuchumi.

Zaidi ya waendesha bodaboda ishirini wameungana na kuanzisha kikundi cha usafirishaji, jambo ambalo limewasaidia kujikwamua kiuchumi, kupunguza utegemezi, na kuwapatia ajira vijana waliokuwa wakikaa mitaani bila shughuli za kufanya.

Pikipiki zilizokabidhiwa kwa Umoja wa maafisa usafirishaji maarufu kama bodaboda katika Kijiji na Kata ya Makere, Picha na Tryphone Odace

Afisa Mtendaji wa Kata ya Makere, Sixmundi Kato, amesema kuwa hadi sasa vijana wamepatiwa mikopo inayozidi shilingi milioni 130, hali iliyochangia kupungua kwa matukio ya uhalifu na kuwahamasisha vijana kujikita katika shughuli halali za kujipatia kipato.

Baadhi ya maafisa usafirishaji wakiendesha pikipiki walizopewa kama sehemu ya mkopo kijikwamua kiuchumi, Picha na Tryphone Odace

Hata hivyo, wito umetolewa kwa vijana kuendelea kuungana na kusajili vikundi vyao kisheria ili waweze kunufaika na mikopo hiyo, huku Serikali ikiendelea kutoa mafunzo ya kuwawezesha katika shughuli za uzalishaji mali.

Sauti ya Mwandishi wetu Kadislaus Ezekiel