Joy FM
Joy FM
18 March 2026, 14:48

Vitendo vya ukatili ambavyo vimeendelea kutokea katika jamii viongozi wa dini wamehimizwa kuendelea kutoa elimu ili kusaidia kudhibiti vitendo hivyo
Na Mwandishi wetu
Mkuu wa Wilaya ya Kigoma Dkt. Rashid Chuachua, ametoa wito kwa viongozi na waumini wa dini ya kiislam na wananchi kwa ujumla kutumia mfungo wa Mwezi Mtukufu wa Ramadhani, kutafakari kuhusu namna wanavyoweza kuendelea kudumisha upendo, mshikamano, amani na utulivu kuanzia ngazi ya familia mpaka ngazi ya Taifa.
Ametoa wito huo kwenye Iftar iliyoandaliwa na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa TAKUKURU mkoa wa Kigoma, ambapo viongozi mbali mbali akiwemo Sheikh Mkuu wa Mkoa wa Kigoma, Sheikh Hassan Kiburwa pamoja na waumini wa dini ya kiislam wameshiriki Iftar hiyo.

Dkt. Chuachua, amesema hayo kufuatia kukithiri kwa vitendo vya ukatili dhidi ya watoto katika maeneo kadhaa ya wilaya ya Kigoma, yakiwemo matukio ya hivi karibuni yaliyotokea kata za Katubuka na Kibirizi katika Manispaa ya Kigoma Ujiji, ambapo Mkuu huyo wa Wilaya ya Kigoma amesisitiza ulinzi kwa watoto.
Aidha Mkuu wa Wilaya ya Kigoma Dkt. Rashid Chuachua, ametoa wito kwa wananchi wilayani humo kuwatumia Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa TAKUKURU mkoa wa Kigoma kama rafiki ili kufichua matendo mbali mbali yanayoashiria rushwa.
Akizungumza wakati wa Iftar hiyo Sheikh Mkuu wa Mkoa wa Kigoma, Sheikh Hassan Idd Kiburwa, ameishukuru TAKUKURU kwa kuandaa Iftar hiyo, lakini akatumia nafasi hiyo kuwaomba waislam kuyachukua mema yote waliyoyaishi katika mwezi Mtukufu wa Ramadhani na kuyaendeleza katika miezi mingine inayofuata ili kuendelea kuwa watu wazuri.

Kwa upande wake Naibu Mkuu wa TAKUKURU mkoa wa Kigoma, John Mgallah, amesema kupitia huduma ya TAKUKURU RAFIKI, wameendelea kushirikiana na wadau mbali mbali kujua changamoto zilizopo na kuzipatia ufumbuzi.
