Joy FM
Joy FM
18 March 2026, 13:42

Urejeshwaji wa mikopo inayotolewa na Halmashauri unasidia kuweza kuongeza kasi ya utoaji wa mikopo mingine kwa vikundi vingine vyenye uhitaji wa mikopo
Na Hagai Ruyagila
Watendaji wa kata na Mitaa halmashauri ya mji Kasulu Mkoani Kigoma wametakiwa kusimamia na kufuatilia kwa karibu urejeshwaji wa mikopo ya asilimia kumi inayotolewa kwa wananchi kupitia Halmashauri mbalimbali Nchini.

Wito huo umetolewa na Mkuu wa Wilaya ya Kasulu, Kanali Isaac Mwakisu, wakati akizungumza na watumishi wa umma wa halmashauri ya Mji Kasulu katika kikao kazi kilicholenga kujadili utekelezaji wa majukumu yao ya Kila siku
Kanal Mwakisu amewasisitiza umuhimu wa watendaji hao kuwa karibu na Wananchi katika maeneo yao ili waweze kutoa elimu kuhusu ulazima wa kurejesha mikopo hiyo kwa wakati, badala ya kusababisha hasara kwa halmashauri.
Aidha, Kanali Mwakisu ameeleza kuwa iwapo mikopo itatokewa kwa watu wasiokuwa na sifa stahiki, watendaji husika wanapaswa kuwajibika kwa uzembe huo.
Kwa upande wake, Afisa mwandamizi wa TAKUKURU kutoka dawati la uchunguzi wilaya ya Kasulu Alfa Eliyatosha, ameeleza wajibu wa watumishi wa umma katika kuzuia vitendo vya rushwa, akisisitiza uwajibikaji na uadilifu katika utendaji kazi wao.

Naye, afisa mtendaji wa mtaa wa Sinza, kata ya Mwilamvya, Njile Charles, akizungumza kwa niaba ya watendaji wenzake, amesema watahakikisha wanafuatilia kwa karibu urejeshwaji wa mikopo hiyo ili kuepuka upotevu wa fedha na kuilinda serikali dhidi ya hasara.