Joy FM
Joy FM
17 March 2026, 15:59

Vitongoji 316 Mkoani Kigoma vinatarajia kupata umeme ambapo serikali imetenga zaidi ya shilingi bilioni 54 ili kusaidia wananchi kujikwamua kiuchumi
Na Mwandishi wetu
Mkuu wa Wilaya ya Kigoma Dkt. Rashid Chuachua, ameishukuru serikali ya awamu ya sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kuimarisha huduma ya upatikanaji wa umeme katika mkoa wa Kigoma, na kwamba hatua hiyo imechangia pakubwa kusukuma mbele kasi ya maendeleo ya mkoa huo.
Amesema kwa miaka mingi Wilaya ya Kigoma na Mkoa wa Kigoma kwa ujumla umekuwa ukipata changamoto kubwa ya umeme iliyotokana na kutounganishwa kwenye gridi ya Taifa, lakini chini ya serikali ya awamu ya sita changamoto hiyo imebaki kuwa historia tu.

Dkt. Chuachua, amesema hayo leo Machi 17, 2026 wakati akimwakilisha Mkuu wa Mkoa wa Kigoma kwenye hafla fupi ya kupokea na kukabidhi magari matano, Bajaji tano na Pikipiki kumi na moja kwa Mameneja wa TANESCO kutoka Wilaya zote za mkoa wa Kigoma.
Aidha Dkt Chuachua amesema kwa kuwa na usafiri imara TANESCO, itaweza kutekeleza majukumu yake kwa urahisi na kutatua changamoto za huduma ya umeme kwa wananchi.

Kwa upande wake, Kaimu Meneja wa TANESCO Mkoa wa Kigoma, Mhandisi Hassan Nganjau, akiongea mara baada ya kukabidhiwa magari, Bajaji na Pikipiki, amesema yataleta tija kwa kurahisha utendaji kazi wao.
Akiongea kwa niaba ya Mameneja wezake Kaimu Meneja wa TANESCO Wilaya ya Kakonko Mercy Mwanga amesema upatikanaji wa usafiri unaenda kutatua changomoto za kuchelewa kufika kutatua changamoto zinazokuwa zimejitokeza kwa wananchi.