Joy FM
Joy FM
17 March 2026, 10:24

Siku chache baada ya ajali ya boti iliyosababisha vifo vya watumishi wa idara ya afya wa Halmashauri ya Wilaya Kigoma, baadhi ya viongozi wa dini na waumini wa kanisa la Anglikana wamesema maisha ya binadamu hapa duniani ni muda na hivyo hawana budi kumrudia mungu
Na Hagai Ruyagila
Askofu wa Kanisa la Anglikana Dayosisi ya Western Tanganyika Mhashamu Emmanuel Bwatta, ametoa salamu za pole kwa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kufuatia vifo vya watumishi saba wa Idara ya Afya waliopoteza maisha baada ya boti walilokuwa wakisafiria kuzama katika Ziwa Tanganyika Mkoani Kigoma.

Askofu Bwatta ametoa salamu hizo wakati wa ibada takatifu ya kuwawekea mikono wanafunzi wa darasa la Kipaimara iliyofanyika katika Kanisa la Anglikana Ebeneza lililopo katika Halmashauri ya Mji Kasulu.
Katika salamu zake, Askofu Bwatta ameungana na Watanzania wote kuomboleza msiba huo na kutoa pole kwa serikali pamoja na familia zilizopoteza wapendwa wao, huku akiomba Mungu awape faraja na nguvu katika kipindi hiki kigumu cha majonzi.

Mkurugenzi wa kanisa la Anglikana Kanda ya Kasulu Mjini, Mchungaji Canon James Bigombo, amesema kanisa linaungana na Askofu Bwatta pamoja na serikali katika kuwaombea wafiwa wote ili Mungu awape uvumilivu na faraja wakati huu wa maombolezo.

Baadhi ya waumini wa Kanisa la Anglikana wilayani Kasulu wamesema wamepokea kwa huzuni taarifa ya vifo hivyo, na wametoa pole kwa familia zilizopoteza ndugu zao pamoja na serikali, wakisisitiza umuhimu wa kumuomba Mungu ili awafariji wote walioguswa na tukio hilo.