Joy FM
Joy FM
13 March 2026, 08:29

Majiko sanifu ni majiko yaliyoboreshwa ili kutumia nishati kama kuni au mkaa kwa ufanisi zaidi na katika jamii nyingi, hasa maeneo ya vijijini na mijini, majiko haya yamekuwa na umuhimu mkubwa kwa maisha ya wananchi kwani majiko sanifu huchangia katika kuboresha maisha ya watu kiuchumi, kiafya na kimazingira.
Na Dotto Josephati
Wananchi Wilayani Kibondo Mkoani Kigoma wametakiwa kuchangamkia fursa ya kununua majiko sanifu yanayotumia mkaa kidogo ili iweze kuwapunguzia gharama za kutumia kuni na mkaa ambapo majiko hayo yana ruzuku ya serikali kwa asilimia 85.
Hayo yamesemwa na Mkuu wa Wilaya ya Kibondo Kanali Agrey Magwaza wakati wa uzinduzi wa majiko hayo katika Kata ya Nyaruyoba ambayo yametengezwa na kampuni ya INVOTEC na kusambazwa na REA ambapo amewahimiza wananchi watakaopata majiko hayo kuyatumia vizuri ili yaweze kuwasaidia kupunguza matumizi ya kuni na mkaa.

Naye mkurugenzi wa taasisi ya Tanzanzania Women Empowerment Network Bi. Frolence Masunga amesema lengo kuu la kutoa majiko hayo ni kumsaidia mwananchi kuepukana na magonjwa yanatokana na matumizi ya nishati chafu ya kupikia na kuendelea kulinda afya za watanzania.

Kwa upande wake, Mwakilishi kutoka REA Bw. Ramadhan Ramadhan amesema majiko hayo yana ubora wa hali ya juu ambalo litamsaidia mwananchi kutumia mkaa kidogo na wanaendelea kuhamasisha wananchi kutumia mkaa mbadala kwaajili ya kuendelea kutunza mazingira.