Joy FM
Joy FM
12 March 2026, 15:02

Mkoa wa Kigoma umefanikiwa kupunguza kiwango cha upotevu wa mazao wakati na baada ya kuvuna kutoka asilimia 11% mwaka 2023 hadi kufikia asilimia 8%, ya sasa.
Na Hagai Ruyagila
Wakulima wa Kata ya Nyumbigwa katika Halmashauri ya Mji Kasulu Mkoani Kigoma wamesema uwepo wa Mradi wa Kilimo Tija Kigoma (KITIKI) umesaidia kuongeza tija katika uzalishaji wa mazao ya mahindi alizeti na maharage kwa kuzingatia kanuni bora za kilimo.
Mradi wa Kilimo Tija Kigoma KITIKI unafadhiliwa na serikali ya korea kusini KOICA na kutekelezwa na mashirika ya world vision Tanzania na Goodneighbors chini ya usimamizi wa shirika la Mpango wa chakula Duniani (WFP) na unatekelezwa katika halmashauri ya mji kasulu, halmashauri ya wilaya ya Kibondo, halmashauri ya wilaya ya Kasulu na halmashauri ya wilaya ya Kakonko mkoani Kigoma.

Mradi huo umeendelea kuleta matokeo chanya katika uzalishaji na kuongeza kipato cha mkulima kama wanavyoeleza wakulima kutoka kikundi cha wakulima nyanguge kata ya nyumbigwa wakati wa maadhimisho ya siku ya mkulima shambani.
Akitoa taarifa ya mradi huo, Mwakilishi wa Meneja wa Mradi wa Kilimo Tija Kigoma (KITIKI) Samson Katabila amezungumzia namna mradi huo ulivyoweza kuwanufaisha wakulima zaidi ya elfu 19 Katika halmashauri zote ambako mradi huo unatekelezwa lengo ikiwa ni kuhakikisha wakulima wanapata manufaa kupitia mazao wanayozalisha.

Kaimu Mkuu wa kitengo cha Kilimo mifugo na Uvuvi halmashauri ya Mji Kasulu Zephania Sodya amewataka wakulima waliopatiwa mafunzo kutoa elimu kwa wakulima wengine ili waachane na kilimo cha mazoea ili kuleta maendeleo katika sekta ya kilimo.

Mwakilishi wa Diwani wa kata ya Nyumbigwa, Yasini Ntimanya amewasihi wakulima kuendelea kutumia mafunzo hayo kuongeza uzalishaji wa mazao.
