Joy FM
Joy FM
11 March 2026, 15:23

Barabara ni miundombinu muhimu sana katika maisha ya binadamu na maendeleo ya taifa kwani huwezesha usafiri wa watu na usafirishaji wa bidhaa kutoka sehemu moja hadi nyingine, hata hivyo, wakati wa mvua nyingi barabara nyingi huharibika na kupata mashimo, matope au kukatika kabisa hivyo kukarabati barabara zilizoharibika kwa sababu ya mvua ni jambo la muhimu sana.
Na Orida Sayon
Wananchi katika Kata ya Kalinzi halmashauri ya Wilaya ya Kigoma wameomba serikali kukarabati miundombinu ya barabara ya Kalinzi-Matyazo ili waweze kuondokana na changamoto za usafiri na usafirishaji inayowakabili kwa sasa.
Barabara ya Kalinzi –Matyazo iliyopo kata ya kalinzi ni moja barabara muhimu sana inayotumiwa na watu wanaotoka zaidi ya vijiji vinne kwa ajili ya usafiri na usafirishaji wa bidhaa kubwa zaidi ikiwa ni barabara nyeti inayotumiwa na wagonjwa kutoka sehemu mbalimbali za mkoa wa kigoma kufika katika kituo cha afya na malezi ya watoto Matyazo.

Wananchi wa kata hiyo wanakabiliwa na kero ya ubovu wa miundombinu ya barabara hiyo ambayo imekuwa kikwazo kikubwa kinachokwamisha shughuli mbalimbali katika kijiji cha matyazo hasa kipindi cha mvua.
Diwani wa kata hiyo Mh. Ignus Helanya amesema miongoni mwa sababu zilizopelekea uharibifu wa barabara ni pamoja na ukosefu wa mifereji stahiki ya kupitisha maji pindi mvua zinaponyesha.
Aidha amesema serikali ina mkakati wa kujenga barabara hiyo kwa kiwango cha lami ili kurahisisha shughuli za usafiri na usafirishaji.
