Joy FM
Joy FM
4 March 2026, 15:45

Usawa wa kijinsia ni hali ambapo wanawake na wanaume wanapata haki, fursa na rasilimali kwa usawa bila kubaguliwa na ni msingi muhimu wa haki za binadamu na maendeleo ya jamii yoyote.
Na Orida Sayon
Katibu tawala Mkoa wa Kigoma Hassan Rugwa amesema serikali na wadau wa maendeleo wataendelea kujenga hamasa na ushiriki wa jamii katika kuchangia na kuleta usawa wa kijinsia na uwezeshaji wa wanawake.
Mh. Rugwa ametoa kauli hiyo wakati akizungumza na waandishi wa habari kuelekea kilele cha maadhimisho ya siku ya wanawake duniani ambapo kimkoa yatafanyika wilayani Kakonko na kuwa utekelezaji wa mipango, sheria na sera za kitaifa na kisekta kuhusu maswala ya kijinsia na uwezeshaji wanchi kiuchumi, kutaimarisha mifumo na hamasa ya kijamii na kuleta usawa kwa kuongeza msukumo wa wanawake kushiriki katika uongozi na vyombo vya kutolea maamuzi.

Mhe, Rugwa amesema katika maadhimisho ya wiki ya wanawake iliyoanza March mosimwaka huu, Halmashauri na Wilaya zote zimeshiriki katika kufanya shughuli mbalimbali za kijamii ambapo pia amewataka wananchi kujitokeza kushiriki katika maadhimisho ya siku ya wanwake duniani.
Kwa upande wake, Afisa maendeleo ya jamii Mkoa wa Kigoma Msafiri Nzunuri ameendelea kutoa hamasa kwa wanawake kujitokeza kwa wingi kuchangamkia fursa za kiuchumi zinazotolewa katika maeneo yao.

Maadhimisho ya siku ya wanawake Duniani hufanyika ifikapo March 8, kila mwaka na maadhimisho haya mwaka huu kwa Tanzania yamebebwa na Kaulimbiu ya haki na usawa kwa wanawake na wasichana ni msingi jumuishi ili kufikia Dira ya maendeleo ya 2050.