Joy FM
Joy FM
27 February 2026, 16:24

Ardhi ni rasilimali muhimu sana katika maisha ya mwanadamu na maendeleo ya taifa kwa ujumla, lakini migogoro ya ardhi imekuwa ikijitokeza mara kwa mara katika jamii kutokana na sababu mbalimbali ikiwemo mipaka ya mashamba, umiliki wa viwanja, urithi, na matumizi yasiyo rasmi ya ardhi.
Na Lucas Hoha
Ofisi ya Mkuu wa Wilaya ya Kigoma imeanzisha kliniki maalumu ya kutatua migogoro ya ardhi kwa wananchi ili kupunguza malalamiko ya wananchi kuhusu migogoro ya ardhi ambayo imekuwa ikiwakabili wananchi
Jitihada mbalimbali zimeendelea kuchukuliwa na serikali ili kuweka matumizi bora ya ardhi kwa lengo la kupunguza migogoro hiyo ya ardhi.

Akizungumza na waandishi wa habari leo, Mkuu wa Wilaya ya Kigoma Dkt. Rashird Chuachua amesema kliniki hiyo itahusisha watumishi wa halmashauri zote mbili za Wilaya ya Kigoma na Kamishina msaidizi wa Mkoa wa Kigoma anayehusika na masuala ya ardhi.
Chuachua amesema lengo la kliniki ni kutatua migogoro ya ardhi ya muda mrefu ambapo amewataka wananchi wenye changamoto kufika ili kuhakikisha migogoro yao inapata suluhisho.
Utatuzi wa migogoro ya ardhi ni jambo la msingi katika kujenga jamii yenye amani, haki, na maendeleo endelevu na ni wajibu wa serikali na wananchi kushirikiana kuhakikisha migogoro inatatuliwa kwa njia ya kisheria na kwa haki ili kulinda rasilimali hii muhimu kwa kizazi cha sasa na kijacho.