Joy FM

Ukarabati MV Liemba wafikia asilimia 55 Kigoma

19 February 2026, 15:44

Naibu Waziri wa Uchukuzi akipkea maelezo kutoka kwa Meneja wa bandari ya Kigoma kuhusu ukarabati wa MV Liemba, Picha na Tryphone Odace

Serikali kupitia Wizara ya uchukuzi imesema haitosita kuchukua hatua za kisheria kwa wasimamizi wanaopewa dhamana ya kusimamia miradi ya maendeleo ambao wanashindwa kuendana na kasi ya serikali katika utekelezaji na ukamilishaji wa miradi kwa wakati

Na Tryphone Odace

Naibu Waziri wa uchukuzi Mh. David Kihenzile ameeleza kuridhishwa na ukarabati unaoendelea  wa Meli ya MV Liemba unayotajwa kukamilika kwake kutarahisha shughuli za usafirishaji ndani ya ziwa Tanganyika.

Akizungumza mara baada ya ziara ya kutembelea bandari ya Kigoma na kujionea ukarabati wa meli hiyo, Naibu Waziri Kihenzile amesema kuwa dhamira ya serikali ni kuhakikisha inarejesha usafiri wa meli ndani ya ziwa Tanganyika na kukuza uchumi wa taifa na wananchi kwa ujumla.

Sauti ya Naibu Waziri wa uchukuzi Mh. David Kihenzile

Awali akitoa taarifa ya ukarabati wa MV Liemba, Mhandisi wa ukabati wa meli hiyo  Luteni Kanali Elias John amesema ukarabati wa meli hiyo umefikia asilimia 55 na wanategemea kufikia mwezi julai utakuwa umekamilika.

Sauti ya Mhandisi wa ukabati wa meli hiyo  Luteni Kanali Elias John

Kwa upande wake, Mwakilishi wa Mkuu wa Mkoa Kigoma, ambaye ni Katibu tawala Wilaya Kigoma Mganwa Nzota amesema miradi inayotekelezwa na serikali hasa iliyopo chini ya Wizara ya uchukuzi itasaidia kuufungua mkoa wa Kigoma na kukua kiuchumi.

Sauti ya Katibu tawala Wilaya Kigoma Mganwa Nzota

Naye Kaimu Meneja Kampuni za Meli Tanzania tawi la Kigoma Amfrey Daniel amesema kukamilika kwa meli ya MV Liemba kutasaidia mzunguko wa biashara na kuunganisha na mataifa mengine kwa uharaka.

Sauti ya Kaimu Meneja Kampuni za Meli Tanzania tawi la Kigoma Amfrey Daniel