Joy FM
Joy FM
9 February 2026, 16:16

Watendaji wa idara ya ardhi Mkoani Kigoma wametakiwa kufanya kazi kwa bidii na kutatua migogoro ya adhi ambayo imeendelea kujitokeza kwenye jamii
Na Mwandishi wetu
Katibu Tawala Mkoa wa Kigoma Hassan Rugwa, amewataka watendaji wa Idara ya Ardhi mkoani hapa kuongeza kasi katika utekelezaji Sera ya Maendeleo ya Makazi ya Taifa pamoja na Sheria ya Mipango miji ili kupunguza migogoro ya ardhi isiyokuwa ya lazima kwa sasa na siku zijazo.
Rugwa ametoa kauli hiyo alipokabidhi vitendea kazi vilivyotolewa na Serikali kupitia Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa watendaji wa Idara hiyo katika Ofisi ya Kamishna wa Ardhi Mkoa, Baraza la Ardhi na Nyumba Wilaya ya Kigoma pamoja na Halmashauri Nane za Mkoa.

Amesema Idara hiyo inajukumu kubwa la kutatua migogoro ya Ardhi na kuifanya jamii kuepuka mivutano isiyokuwa ya lazima na mbinu mojawapo ya kutatua changamoto hiyo ni pamoja na kuhakikisha uhamishaji wa umiliki wa ardhi unazingatia haki na kufanyika kwa usahihi.
Amesema kwa sasa maeneo mengi ya mkoa yanaendelea kukua, hivyo Idara zinapaswa kuandaa na kutekeleza mipango ya matumizi bora ya ardhi katika miji na vijiji, sambamba na upimaji na ugawaji wa ardhi katika maeneo mapya badala ya kuwaacha wakazi kujitwalia ardhi bila kuzingatia Sheria na taratibu zilizopo.
Aidha amewataka watendaji hao kuepuka rushwa na makosa yasiyo ya lazima wakati wa utendaji kazi wao na kuyafanyia kazi kwa haraka makosa yote yatakayojitokeza ili kuwapunguzia wanachi kero zitolanazo na migogoro ya ardhi.
Vifaa vilivyotolewa ni pamoja na Kompyuta 18, Printa 9, UPS 20, Kompyuta za GIS 2, Simu za IP 2 pamoja na Scanner moja.