Joy FM
Joy FM
5 February 2026, 12:34

Miundombinu ya barabara ni nguzo muhimu katika maendeleo ya kijamii na kiuchumi kwa jamii yoyote kwani barabara bora huwezesha usafiri wa watu na bidhaa, kuimarisha biashara, na kurahisisha upatikanaji wa huduma muhimu kama elimu, afya na usalama hali inayosababisha usumbufu kwa wananchi na kudhoofisha shughuli za kiuchumi.
Na Orida Sayon
Halmashauri ya Manispaa ya Kigoma Ujiji imeazimia kufanya manunuzi wa mitambo ya ukarabati wa miundombinu ya barabara ikiwemo katapila kwa lengo la kutatua changamoto ya ubovu wa miundombinu ya barabara.
Maazimio hayo yamefanyika katika baraza la madiwani baada ya kuona changamoto ya ubovu wa miundombinu ya barabara Manispaa ya Kigoma Ujiji kuwa kubwa na inagharimu shughuli za usafiri na usafirishaji wa wananchi na bidhaa mbalimbali.

Kutokana na Mapendekezo yaliyowasilishwa na kamati ya fedha na uongozi madiwani wakapendekeza kununua katapila ili kuondoa adha ya miundombinu mibovu ya barabara inayocheleweshwa na bajeti finyu inayotoka TARURA.
Akisoma maazimio ya baraza la madiwani, Mstahiki Meya wa Manispaa ya Kigoma ujiji Mhe. Mussa Maulidi amemuagiza Mkurugenzi wa manispaa hiyo kusimamia maazimio yao ikiwa ni pamoja na ununuzi wa katapila hilo.
Kwa upande wake, Mkurugenzi wa manispaa ya kigoma ujiji Mhe. Kisena Mabuba mbali na kueleza mkakati wa ununuzi wa katapili (grader) ameshauri kuendelea kushirikiana na wataalamu kuandika miradi itakayokuwa sehemu ya kudhibiti miundombinu mibovu ya barabara.