Joy FM

Watumishi Kasulu wapanda miti siku ya kuzaliwa Rais Dkt. Samia

27 January 2026, 15:42

Baadhi ya watumishi wa halmashauri ya Mji Kasulu wakiwa wameshika miti kujiandaa kuipanda, Picha na Hagai Ruyagila

Jamii katika Halmashauri ya Mji Kasulu Mkoani Kigoma imetakiwa kuwa na desturi ya kupanda miti katika maeneo yanayowazunguka

Na Hagai Ruyagila

Watumishi wa Halmashauri ya Mji Kasulu mkoani Kigoma wameadhimisha siku ya kuzaliwa ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mh Dkt Samia Suluhu Hassan kwa zoezi la upandaji miti katika Hospitali ya Mji Kasulu, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuendelea kutunza na kuboresha mazingira ya hospital hiyo.

Akizungumza wakati wa zoezi hilo, Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji Kasulu Mwl, Vumilia Simbeye amesema wamemuunga mkono Rais Samia katika siku hiyo kwa kupanda miti hivyo watumishi pamoja na wananchi wote wanatakiwa kuwa wazalendo kwa kufanya hivyo.

Mkurugenzi wa halmashauri ya Mji Kasulu akipanda mti aina ya mparachichi katika eneo la hospital ya Mji Kasulu, Picha na Hagai Ruyagila

Pia amesema kupanda miti kwa wingi ili kuendelea kutunza mazingira ni miongoni mwa mikakati muhimu ya halmashauri katika kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi pamoja na kuhakikisha kunakuwepo mazingira bora na salama kwa jamii.

Sauti ya Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji Kasulu Mwl. Vumilia Simbeye

Mwenyekiti wa Halmashauri ya Mji Kasulu Mh. Ayubu Ngalaba  amewahimiza wananchi na taasisi mbalimbali kuiga mfano huo kwa kupanda na kutunza miti katika maeneo yao, akisisitiza kuwa utunzaji wa mazingira ni jukumu la kila mmoja na una mchango mkubwa katika maendeleo endelevu ya jamii.

Sauti ya Mwenyekiti wa Halmashauri ya Mji Kasulu Mh. Ayubu Ngalaba
Mkurugenzi wa halmashauri ya Mji Kasulu akizungumza na watumishi wa halmashauri hiyokabla ya kuanza zoezi la upandaji miti aina miparachichi, Picha na Hagai Ruyagila

Afisa Mazingira wa halmashauri hiyo, Bw. Wambura Mniko amesema kuwa miti hiyo aina ya miparachichi iliyopandwa italeta faida mbalimbali ikiwemo kuboresha hali ya hewa, kutunza mazingira ya hospitali, pamoja na kutoa matunda ambayo yatakuwa na manufaa kwa wagonjwa na watumishi wa hospitali hiyo.

Sauti ya Afisa Mazingira wa halmashauri hiyo, Bw. Wambura Mniko
Afisa mazingira wa halmashauri ya Mji Kasulu, Picha na Hagai Ruyagila

Mganga Mfawidhi wa hospitali ya halmashauri ya Mji Kasulu Dkt Japhari Makombe ameishukuru halmashauri kwa kuchagua hospitali hiyo kuwa sehemu ya zoezi hilo muhimu, akisema kuwa miti hiyo itakapokua itasaidia kuboresha mandhari ya hospitali na kutoa hewa safi.

Sauti ya Mganga Mfawidhi wa hospitali ya halmashauri ya Mji Kasulu Dkt Japhari Makombe

Zoezi hilo linaendana na maelekezo ya Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt Samia Suluhu Hassan ya kuhimiza utunzaji wa mazingira na matumizi endelevu ya rasilimali asili.