Joy FM

Madiwani watakiwa kuongeza juhudi ukusanyaji mapato Kasulu

10 December 2025, 14:13

Madiwani wa Halmashauri ya Mji wa Kasulu, Picha na Hagai Ruyagila

Wakati madiwani wa Halmashauri mbalimbali za Mkoa wa Kigoma wakiwa wameshakula kiapo cha kuanza kuwatumikia wananchi kwa kipindi cha miaka mitano msisitizo upo kwenye ukusanyaji wa mapato ili yaweze kusaidia katika utekelezaji wa miradi mbalimbali

Na Hagai Ruyagila

Kaimu Katibu Tawala wa Mkoa wa Kigoma, Elisante Mbilo, amewataka Madiwani wa Halmashauri ya Mji wa Kasulu kuongeza juhudi katika ukusanyaji wa mapato ili kuiwezesha halmashauri hiyo kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi zaidi.

Akizungumza na Madiwani pamoja na watumishi wa serikali wa Halmashauri ya Mji wa Kasulu, Mbilo amewataka viongozi hao kutekeleza wajibu wao kikamilifu na kusimamia ipasavyo ukusanyaji wa mapato ya ndani, akibainisha kuwa hatua hiyo itasaidia kuboresha utoaji wa huduma kwa wananchi.

Sauti ya Kaimu Katibu Tawala wa Mkoa wa Kigoma, Elisante Mbilo
Kaimu Katibu Tawala wa Mkoa wa Kigoma, Elisante Mbilo, Picha na Hagai Rayagila

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Wilaya ya Kasulu, Mbelwa Chidebwe, amewahimiza madiwani kuungana na kushirikiana kwa karibu katika kuhakikisha mapato ya halmashauri yanakusanywa kwa ufanisi ili kuwezesha utekelezaji wa miradi ya maendeleo ndani ya mji.

Sauti ya Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Wilaya ya Kasulu, Mbelwa Chidebwe

Naye Mbunge wa Jimbo la Kasulu Mjini, Profesa Joyce Ndalichako, amesema wananchi wana matarajio makubwa kwa viongozi waliowachagua, hivyo ni muhimu kuwa karibu nao na kusikiliza changamoto zinazowakabili ili kuchukua hatua stahiki.

Sauti ya Mbunge wa Jimbo la Kasulu Mjini, Profesa Joyce Ndalichako

Baadhi ya madiwani wa Halmashauri ya Mji wa Kasulu wametoa ahadi ya kusimamia kwa umakini vyanzo vyote vya mapato kwa kushirikiana na wananchi, ili kuongeza mapato yatakayowezesha halmashauri kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi.

Sauti ya Baadhi ya madiwani wa Halmashauri ya Mji wa Kasulu