Joy FM
Joy FM
10 December 2025, 13:19

Wilaya Kasulu imeendelea kuwa mfano bora kwa uwajibikaji na mshikamano katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo
Na Hagai Ruyagila
Kaimu Mkuu wa Wilaya ya Kasulu Mkoani Kigoma, ambaye ni Katibu tawala wa wilaya ya Kasulu Bi. Theresia Mtelewe, amesema wilaya hiyo imeendelea kuwa mfano bora wa uwajibikaji, usimamizi na mshikamano katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo hali inayoonyesha wazi nguvu ya Serikali, Chama na ushiriki chanya wa wananchi.
Ametoa kauli hiyo wakati wa Kikao cha Halmashauri Kuu ya CCM Wilaya ya Kasulu, kilichofanyika kwa ajili ya kujadili na kupokea taarifa ya utekelezaji wa Ilani ya CCM kwa kipindi cha Juni hadi Novemba 2025.
Akiwasilisha taarifa hiyo, Bi Mtelewe amesema wilaya imeendelea kuimarisha misingi ya maridhiano, mabadiliko, ustahimilivu na ujenzi mpya wa taifa falsafa muhimu zinazobeba uongozi wa Rais wa Awamu ya sita.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Kasulu, Mbelwa Chidebwa, amewataka wabunge na madiwani wa chama hicho kudumisha mahusiano mazuri na watumishi wa serikali. Akiwahimiza umuhimu wa kufanya kazi kwa ushirikiano na kurekebishana kwa staha pale mapungufu yanapojitokeza ili kuimarisha utendaji kazi wao.

Mwenyekiti wa Umoja wa Wanawake wa chama cha Mapinduzi (UWT) Mkoa wa Kigoma, Bi. Agripina Buyogela, amewasihi wenyeviti wa halmashauri zote mbili ya Mji Kasulu na halmashauri ya wilaya ya Kasulu kushirikiana kikamilifu na serikali katika kuwaletea wananchi maendeleo bila kujali itikadi za vyama vyao, akisema maendeleo ni haki ya kila mwananchi.

Mbunge wa jimbo la Kasulu Mjini Profesa Joyce Ndalichako amewasisitiza madiwani wote kuwa chachu kwa wananchi katika kudumisha amani na umoja katika maeneo yao na kutatua changamoto za wananchi wao.
