Joy FM
Joy FM
11 February 2026, 13:36

Jeshi la Polisi wilayani Kasulu mkoani Kigoma limewataka maafisa usafirishaji maarufu bodaboda kutokuwa sehemu ya uvinjifu wa amani.
Na Hagai Ruyagila
Maafisa usafirishaji maarufu kama bodaboda wilayani Kasulu mkoani Kigoma wametakiwa kuepuka kujihusisha na vitendo vya uvunjifu wa amani, na badala yake kushirikiana kwa karibu na vyombo vya ulinzi na usalama katika kufichua wahalifu.
Wito huo umetolewa na Mratibu wa Polisi Jamii wilaya ya Kasulu, Mkaguzi Msaidizi wa Polisi Mkaguzi Willy Lupa, wakati akizungumza na maafisa usafirishaji wilayani humo. Amesisitiza umuhimu wa bodaboda kuwa mstari wa mbele katika kuimarisha ulinzi shirikishi kwa kutoa taarifa za uhalifu pindi wanapobaini vitendo viovu.

Mkaguzi Lupa amesema kuwa baadhi ya maafisa usafirishaji wamekuwa wakijihusisha na vitendo vya kihalifu ikiwemo kukwapua mikoba na simu za wananchi, hali inayochafua taswira na sifa ya waendesha bodaboda kwa ujumla.
Ameongeza kuwa ushirikiano kati ya bodaboda na vyombo vya ulinzi na usalama ni muhimu katika kudhibiti uhalifu na kulinda usalama wa wananchi na mali zao.
Kwa upande wao, baadhi ya maafisa usafirishaji maafuru bodaboda wilayani Kasulu wamekiri kuwepo kwa baadhi ya madereva wanaotumiwa au kujihusisha na vitendo vya kihalifu, huku wakisisitiza kuwa si jambo jema na linapaswa kukemewa.
Wamesema ni wajibu wa kila dereva kutoa taarifa kwa vyombo vya sheria anapobaini vitendo hivyo ili kulinda heshima ya kazi yao.
