Joy FM

Serikali kuwasaka waliohusika na mauaji Uvinza

9 February 2026, 08:18

Mwananchi alinusurika katika tukio la mauwaji ya mtu mmoja, Picha na Ofisi ya mawasiliano Kigoma

Mkuu wa Mkoa wa Kigoma Balozi Simon Sirro, amekemea vikali tabia ya baadhi ya wananchi kujichukulia sheria mkononi sambamba na kujihusisha na uhalifu.

Na Kadislaus Ezekiel

Mkuu wa Mkoa wa Kigoma, Balozi Simon Sirro, amekemea vikali tabia ya baadhi ya wakazi mkoani hapa kujichukulia Sheria mkononi sambamba na kujihusisha na uhalifu huku akisisitiza kuwa, serikali haitosita kuwakamata na kuchukua hatua kali dhidi ya wahusika wa vitendo hivyo.

Mkuu wa Mkoa Kigoma Balozi Simon Sirro akizungumza na wananchi wa Kijiji cha Ilunde, Picha na Ofisi ya mawasilian Kigoma

Balozi Sirro ametoa kauli hiyo  alipozungumza na wakazi katika Kitongoji  cha Ilunde wilayani Uvinza mkoani hapa, kufuatia tukio la kifo cha mtu mmoja aliyefahamika kwa jila la Petro Kabasha (35), aliyeuwawa na watu ambao bado hawajafahamika wakati akilinda eneo la mwekezaji katika eneo tengefu la vitalu vya ufugaji wilayani  humo.

Amesema eneo hilo limekuwa na historia ya migogoro ya muda mrefu ya ardhi ambayo pia imekuwa ikihusisha wakulima na wafugaji,  ambapo amewataka wananchi kutojichukulia sheria mkononi pale inapotokea mivutano kati yao bali waendelee kutumia mifumo ya kisheria kumaliza tofauti zao.

Wananchi wa Kijiji cha Ilende Wilayani Uvinza wakiwa katika mkutano na mkuu wa mkoa, Picha na Ofisi ya mawasiliano Kigoma.

Amelitaka Jeshi la Polisi kuendesha zoezi maalum la kuwasaka watu wote wanaoendesha vitendo vya kihalifu na uvunjifu wa amani katika eneo hilo na kuwapeleka Mahakamani bila kuonea mtu au kuacha baadhi ya wahalifu wakiendelea kusumbua wananchi.

Upande wake Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kigoma Filemon Makungu, amesema uchunguzi unaendelea ili kuwabaini wahusika huku akisisitiza wananchi kushirikiana na Jeshi hilo kwa lengo la kuwafichua wahalifu wote waliohusika na tukio  hilo.

Wananchi wa Kijiji cha Ilende Wilayani Uvinza wakiwa katika mkutano na mkuu wa mkoa, Picha na Ofisi ya mawasiliano Kigoma.

Baadhi ya wakazi katika kitongoji hicho, wameliomba Jeshi la Polisi kuongeza nguvu na kuweka mikakati madhubuti katika kukabiliana na matukio hayo ili kudhibiti vitendo hivyo vya uvunjifu wa amani.