Joy FM
Joy FM
1 December 2025, 12:21

Wadau mbalimbali Wilayani Kasulu Mkoani Kigoma wameshauriwa kuendelea kujitokeza na kuwasaidia watoto wenye uhitaji
Na Hagai Ruyagila
Umoja wa Kikundi cha Watendaji wa Serikali za Mitaa (MEOS) cha Halmashauri ya Mji Kasulu mkoani Kigoma kimetoa msaada wa mahitaji mbalimbali kwa kituo cha Center of Hope. Msaada huo umehusisha sukari, jiko dogo la gesi, gunia la moja la mkaa na sabuni.
Akizungumza wakati wa kukabidhi msaada huo, Mwenyekiti wa watendaji wa serikali za mitaa Halmashauri ya Mji Kasulu Bw. Leonard Lugunguja, ambaye pia ni Afisa mtendaji wa Mtaa wa Tabilugu kata ya Ruhita amesema lengo la kutoa msaada huo ni kuwafariji na kuboresha huduma kwa watoto wanaolelewa katika kituo hicho.

Mratibu wa kikundi hicho Bi. Getruda Busombo amebainisha vitu vilivyotolewa na wanakikundi hao pia akisisitiza hatua hiyo ni sehemu ya kuunga mkono jitihada za kituo katika kuwalea watoto wanaokabiliwa na changamoto mbalimbali za kijamii.

Kwa upande wake, Afisa Mtendaji wa Mtaa wa Kinazi kata ya Ruhita Bw. Moses Joseph akitoa hotuba ya Neno la Mungu, amezungumzia umuhimu wa kuwasaidia wasiojiweza, akieleza kuwa kutoa kwa moyo mmoja kunaleta baraka na faida kubwa kwa jamii.
Naye Meneja wa kituo hicho Bi. Rebecca Rock ametoa neno la shukrani kwa watendaji hao kwa kuonesha upendo kwao.

Katika hafla hiyo watendaji wamepata nafasi ya kuwaombea watoto wa kituoni hapo ili wakue katika mazingira bora yenye furaha, malezi mema na maadili yatakayowasaidia katika maisha yao ya baadae.