Joy FM
Joy FM
28 October 2025, 14:32

Serikali imewataka wazazi na walezi kuhakikisha wanawapa watoto wenye ulemavu nafasi ya kwenda shule ili wapate elimu kama watoto wengine
Na Hagai Ruyagila
Wazazi na walezi Wilayani Kasulu Mkoani Kigoma wametakiwa Kuwapatia fursa watoto wao wenye mahitaji maalumu kushiriki katika shughuli mbalimbali za uzalishaji na kuwapeleka shule ili wapate elimu itakayowasadia kufikia malengo yao.
Jitihada za kutoa Elimu kwa wazazi na walezi pamoja na jamii kwa ujumla kuhusu umuhimu wa kuwapa fursa watoto wao wenye mahitaji maalumu zinaonekana kuzaa matunda kwa kuwa malengo mahususi ni kuhakikisha watoto wenye ulemavu wanapatiwa elimu ambayo itawanufaisha katika maisha yao ya kila siku.

Tabia ya baadhi ya wazazi na walezi kuwafungia majumbani watoto wao wenye mahitaji maalumu inatajwa na Mwenyekiti wa Vyama vya Watu Wenye Ulemavu Wilaya ya Kasulu, Zakayo Nkohozi, kuwa kitendo hicho ni ukatili wa kijinsia, kwani kinawanyima haki ya msingi ya kupata elimu na fursa nyingine za maendeleo.
Afisa Elimu (Elimu Maalumu) wa Halmashauri ya Mji Kasulu, Mwl. Salvatory Kitogwe, amesema Serikali imeweka mikakati mbalimbali ya kuhakikisha watoto wote, wakiwemo wenye ulemavu, wanapata Elimu bora kutokana na miundombinu yao kuwa rafiki.

Mwakilishi wa wazazi wa watoto wenye ulemavu wilayani Kasulu Elizabeth Kamenya amesema kila mtoto anakipawa chake kutoka kwa mwenyezi Mungu hivyo jukumu la wazazi ni kuhakikisha wanaonyesha ushirikiano na kutoa nafasi kwa watoto wao wenye ulemavu kupatiwa elimu ili wapate nafasi ya kuonyesha uwezo wao.